Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 6 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 84 2019-11-12

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-

Kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu ya madeni mbalimbali ya wazabuni wanaoidai Serikali:-

Je, Serikali imefikia hatua zipi katika kuhakikisha inalipa madeni ya wazabuni nchini?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Emanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kulipa madeni yaliyohakikiwa na kukubaliwa kupitia bajeti inayoidhinishwa na Bunge lako tukufu. Kati ya mwaka 2016/ 2017 na robo ya kwanza ya mwaka 2019/2020, Serikali imetoa jumla ya shilingi 2,528,619,142,345.21 kulipa madeni yaliyohakikiwa ya watumishi, wazabuni, wakandarasi/wahandisi washauri, watoa huduma na madeni mengineyo. Kati ya kiasi hicho, jumla ya shilingi 379,072,545,151.14 zimetolewa kulipa madeni ya wazabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kupunguza madeni, ikiwa ni pamoja na kutenga fedha kwenye bajeti kila mwaka kwa ajili ya kulipa madeni yaliyohakikiwa na kukubaliwa, kuweka sheria na kanuni zake kama vile Sheria ya Bajeti Sura 439 na Kanuni zake; Sheria ya Manunuzi, Sura 410; Sheria ya Fedha, Sura 348 na kutoa miongozo na maelekezo mbalimbali ikiwemo Waraka Na.1 wa Mlipaji Mkuu wa Serikali unaotolewa kila mwaka kuhusu utekelezaji wa bajeti na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti unaotolewa kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ulipaji wa madeni yaliyohakikiwa, Serikali imeandaa mkakati wa kulipa madeni yaliyohakikiwa na kuzuia ulimbikizaji wa madeni. Madeni yanayohusika kwenye mkakati huo ni yaliyozalishwa na Wizara, Idara Zinazojitegemea na Sekretarieti za Mikoa yakiwemo madeni ya watumishi, wazabuni na watoa huduma, pamoja na madeni ya wakandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na changamoto ya madeni, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya kulipa madeni yaliyohakikiwa kwa kuzingatia mwelekeo ulioandaliwa wa kulipa madeni hayo kulingana na upatikanaji wa mapato.

Aidha, lengo la Waraka Na.1 wa Mlipaji Mkuu unaotolewa kila mwaka ni kuiwezesha Serikali kufikia malengo yake ya kudhibiti madeni na kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati ikiwemo kuzuia uzalishaji na ulimbikizaji wa madeni.