Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 6 Water and Irrigation Wizara ya Maji 80 2019-11-12

Name

Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza:-

Je, ni kwa kiasi gani Serikali imeweka mikakati ya kuhamasisha uvunaji wa maji ya mvua ili kupunguza tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi hasa ikizingatiwa kuwa Tanzania kijiografia ipo katika ukanda wenye mvua za kutosha?

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI, alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athuman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, chanzo kimojawapo katika kuongeza uhakika wa upatikanaji wa maji kwa wananchi ni maji ya mvua. Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ilizielekeza Mamlaka za Serikali za Mtaa kutunga sheria ndogo ndogo ili kuhamasisha na kushauri kuwa nyumba zote zinazojengwa ziwekewe miundombinu kwa ajili ya uvunaji wa maji ya mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa uhaba wa maji bado ni changamoto katika nchi yetu, Serikali inaendelea kuhimiza na kuhamasisha jamii kwa kutoa elimu ya utaratibu wa uvunaji wa maji ya mvua kwa kutumia njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na ujenzi wa mabwawa, malambo na uvunaji wa maji ya paa. Katika utekelezaji wa Programu ya kuendeleza Sekta ya Maji nchini, uhamasishaji umefanyika kwa kujenga matenki ya mfano ya kuvuna maji ya mvua katika maeneo ya shule na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Maji imeandaa Mwongozo wa Uvunaji wa Maji ya Mvua ambao utasambazwa na kutumika nchi nzima. Mwongozo huo umeainisha mbinu mbalimbali za kuvuna maji ya mvua katika Kaya na Taasisi. Mwongozo utatumika katika kupanga, kusanifu, kujenga na uendeshaji na matengenezo ya miundombinu ya uvunaji wa maji ya mvua. (Makofi)