Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 5 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 60 2019-11-11

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:-

Je ni nini maana ya dhana ya uchumi kukua ukioanisha na maisha ya wananchi?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali Ia Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, dhana ya uchumi kukua ikioanishwa na maisha ya wananchi inaweza kutafsiriwa katika dhana kuu mbili. Dhana ya kwanza ni kwa kuangalia upatikanaji, ubora na gharama ya huduma za jamii zinazotolewa na Serikali. Baadhi ya huduma hizo ni pamoja na elimu, afya, maji, umeme na miundombinu ya usafiri na usafirishaji. Mathalani, kutokana na uboreshaji wa miundombinu ya barabara, muda na gharama za usafiri na usafirishaji wa bidhaa zimepungua, sambamba na gharama za matengenezo ya vyombo vya usafiri na usafirishaji. Aidha, upatikanaji wa huduma za afya karibu na wananchi umepunguza kwa kiasi kikubwa adha na gharama ya matibabu kwa wananchi. Pia, ugharamiaji wa elimu msingi bila malipo na utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu ni miongoni mwa matokeo ya kukua kwa uchumi. Kwa muktadha huu, ni muhimu kutafsiri dhana ya ukuaji wa uchumi na maisha ya wananchi kwa kuangalia kiwango cha upatikanaji, ubora na gharama za huduma muhimu za jamii zinazotolewa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, dhana ya pili ya kutafsiri ukuaji wa uchumi na maisha ya wananchi ni ushiriki wa wananchi wenyewe katika shughuli za kiuchumi. Ukuaji wa uchumi ni matokeo ya wananchi kushiriki moja kwa moja kwenye shughuli za uzalishaji mali na huduma. Wananchi wanaoshiriki moja kwa moja kwenye shughuli za kiuchumi hufikiwa moja kwa moja na matokeo chanya ya ukuaji wa uchumi ikilinganishwa na wale ambao wapo nje ya mfumo wa uzalishaji. Aidha, wananchi wanaoshiriki moja kwa moja kwenye shughuli za kiuchumi wananufaika kwa tafsiri ya dhana zote mbili; yaani kupitia huduma za jamii zinazotolewa na Serikali yao pamoja na matokeo ya moja kwa moja ya shughuli wanazofanya.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kufanya jitihada za dhati kabisa kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na biashara, ili kila Mtanzania aweze kutumia kikamilifu fursa zilizopo kushiriki katika shughuli za uzalishaji mali na huduma. Miongoni mwa hatua madhubuti zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ni pamoja na utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Kuboresha Mazingira ya Kufanya Biashara Nchini. Lengo ni kuhakikisha kwamba, tunapunguza kwa sehemu kubwa gharama za uwekezaji na kufanya biashara ili kuvutia wawekezaji mahiri katika sekta mbalimbali, hususan viwanda vinavyotumia malighafi za ndani. Ni matarajio ya Serikali yetu kuwa, uwekezaji katika viwanda utaongeza ajira na uzalishaji katika Sekta ya Kilimo, sekta ambayo huajiri idadi kubwa ya watu hapa nchini, lakini imekuwa ikikua kwa kasi ndogo na hivyo kuwa na mchango mdogo katika kupunguza umaskini wa wananchi walio wengi, hususan wakulima.