Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 4 Energy and Minerals Wizara ya Madini 53 2019-11-08

Name

Yosepher Ferdinand Komba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Katika Kijiji cha Sakale, Kitongoji cha Kwempasi, Tarafa ya Amani katika Wilaya ya Muheza wananchi waligundua uwepo wa madini na shughuli za uchimbaji zilianza, lakini baada ya muda Serikali imefunga machimbo yale:-

Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kufungua machimbo hayo ili wachimbaji wadogo hususan vijana wazawa waweze kunufaika.

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinard Komba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) ikishirikiana na wadau wa maendeleo ilifanya utafiti na ulibaini uwepo wa madini ya dhahabu katika Vijiji vya Mindu, Amani, Tengeni, Segoma, Mbambara, Sakale, Muheza na Korogwe. Pia Wilaya ya Muheza ina madini ya ujenzi kama vile mchanga na mawe katika Vijiji vya Magila, Kilapula, Kwakifua, Mhamba, Furaha na Tanganyika na madini ya garnet, ruby na sapphire katika Kijiji cha Misozwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli machimbo yaliyokuwa yakiendelea katika Kijiji cha Sakale yalifungwa tarehe 2 Oktoba, 2018 baada ya timu ya watalaam kubaini uchimbaji huo kutokuzingatia Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na Marekebisho yake ya mwaka 2017. Aidha, Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004 na kanuni zake haziruhusu kufanya uchimbaji katika vyanzo vya maji ili kuzuia kemikali ya zebaki na uchafu utokanao na uchenjuaji kuingia kwenye mito ambayo inamwaga maji kwenye Bwawa la Bayani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji huo ulikuwa unafanyika katika vilima vya Kwempasi na Nelusanga ambapo uchimbaji unaweza kutiritirisha majitaka na udongo kutoka juu ya vilima na kuingia katika bonde la Mto Kihara ambao ni moja ya chanzo cha Bwawa la Bayani linalotumiwa na wakazi zaidi ya laki 500 katika Wilaya ya Korongwe, Muheza na Jiji la Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu ya watalaam ilishauri mwekezaji mzawa au mgeni anaweza kuruhusiwa kuchimba madini hayo kwa kutumia leseni ya uchimbaji mkubwa na kuweza kufanya tathimini ya kimazingira (EIA) na kuwashirikisha wadau wote muhimu kabla ya kuanza uchimbaji ili kuzuia uharibifu huo wa mazingira.