Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 45 2019-11-08

Name

Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-

Utalii wa baharini (Diving unakua kwa kasi sana na hakuna chuo kinachotoa elimu hiyo hapa nchini:-

Je, Serikali haioni kuwa tunapoteza ajira nyingi kwa vijana wetu?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafunzo ya Uzamiaji kwenye Maji kwa kutumia vifaa vya kupumulia ndani ya maji (Self Contained Underwater Breathing Apparatus – SCUBA Diving) yanatolewa nchini na Chuo cha Wakala wa Mafunzo ya Uvuvi Tanzania – FETA, Kampasi ya Mbegani, iliyopo Bagamoyo. Kwa sasa chuo kinakabiliwa na uchache wa watumishi wenye utaalam kwenye fani hiyo. Aidha, wakufunzi watatu (3) wapo nje ya nchi (Uingereza wawili na Uturuki mmoja) kwa ajili ya mafunzo katika fani hizo ambapo wanatarajiwa kurejea nchini mwaka 2020/21. Baada ya kurejea kwa wakufunzi hao, chuo kitaendelea kutoa mafunzo hayo mwakani. Aidha, vyuo vyote vina kozi ya lazima ya Swimming na Snorkelling ambayo inahusisha kipengele cha diving kwa wanafunzi wanaochukua masomo ya Sayansi ya Viumbe Maji (Aquatic Science).

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto hiyo, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia taasisi yake ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu inaendelea kuhamasisha Sekta Binafsi kuanzisha vituo vya uzamiaji (Diving Centres) ambapo sambamba na vituo hivyo kutoa elimu ya uzamiaji kwa wananchi katika maeneo ya fukwe za Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi. Hatua hii itawezesha kuhudumia watalii wa ndani na nje ya nchi pamoja na kuongeza kipato kwa wananchi na pia kusaidia kuimarisha aina hiyo ya utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa vituo vya Sekta binafsi vinavyotoa huduma ya uzamiaji pamoja na elimu ya uzamiaji nchini vinapatikana katika maeneo ya Hifadhi ya Bahari ya Mafia, Mkoani Pwani (Big Blue, Shamba Kilole na Mafia Island Dive); Maeneo tengefu ya Mkoa wa Dar es Salaam (Yatch Club na White Sands); Hifadhi ya Bahari ya Silikanti Tanga (Kasa Dive na Fish Eagle Point) na Fukwe za Mkoa wa Mtwara (Mikindani Diving Centre).