Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 3 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 35 2019-11-07

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. MARY D. MURO (K.n.y. MHE. AIDA J. KHENAN) aliuliza:-

Je, ni lini Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) litajenga nyumba za bei nafuu ambazo wananchi wenye hali ya chini wataweza kununua?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limekuwa likitekeleza miradi ya ujenzi wa nyumba kwa kufuata Mpango Mkakati wa Miaka 10 unaoanza 2015/2016 - 2024/2025. Pamoja na Shirika kutekeleza mpango mkakati huo, Shirika limekuwa na miradi ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa kipato cha chini wamekuwa wakishindwa kumudu gharama za nyumba hizo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo gharama kubwa ya kununua ardhi, riba ya mikopo na gharama za uwekaji wa miundombinu katika maeneo ya miradi. Ili Shirika liweze kujenga nyumba za gharama nafuu hususani kwa ajili ya wananchi wa kipato cha chini, mamlaka husika zinatakiwa kuwezesha upatikanaji wa ardhi, uwepo wa miundombinu ya umeme, maji, barabara na riba nafuu ya mikopo ya taasisi za fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017 Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika ziara Mkoa wa Mtwara aliagiza kuwa Halmashauri zote nchini zitoe ardhi kwa Shirika la Nyumba la Taifa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu na pia taasisi zinazohusika na miundombinu ziweke miundombinu hiyo kwenye maeneo ya miradi ya shirika ili kupunguza gharama ya nyumba hizo. Kufuatia utekelezaji wa maelekezo hayo, bei ya nyumba katika baadhi ya miradi imeshuka kwa kiasi kikubwa. Mfano, bei ya nyumba katika mradi wa Chatur, Wilaya ya Muheza imeshuka mpaka shilingi milioni 24.6 ikilinganishwa na bei ya miradi ya awali mfano Ilembo, Katavi ambayo ilikuwa inauzwa milioni 30.6; Mlole Kigoma milioni 34.2; na Mtanda, Lindi milioni 33.6. Tunatoa rai kwa Halmashauri zingine za Miji na Wilaya kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais ili waweze kujengewa nyumba za gharama nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi, shirika linadhamiria kujikita zaidi katika ujenzi wa nyumba za kupangisha ili kuwafikia wananchi wengi zaidi wasio na uwezo wa kununua nyumba. Kwa kuanzia nyumba hizo za kupangisha zitajengwa katika Jiji la Dodoma eneo la Chamwino ili kukidhi mahitaji yaliyopo hususan kwa watumishi wa Serikali.