Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 32 2019-11-07

Name

Rose Kamili Sukum

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA (K.n.y. MHE. ROSE K. SUKUM) aliuliza:-

Mpango wa Serikali kupeleka fedha za afya moja kwa moja kwenye Vituo vya kutolea huduma za Afya umesaidia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na stahiki za watumishi, lakini Waganga Wafawidhi hufanya kazi za Wahasibu na Maafisa Manunuzi na hivyo kusababisha kutotoa huduma kwa wagonjwa kwa wakati:-

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kuajiri Wahasibu na Maafisa Manunuzi kwa kila Zahanati?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SRIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Rose Kamil Sukum, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Mpango wa Serikali wa kupeleka fedha za afya moja kwa moja kwenye Vituo vya kutolea huduma za Afya umesaidia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na stahiki za watumishi. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali iliajiri kwa mkataba Wahasibu Wasaidizi 535 na kuwapanga katika Vituo vya Afya vya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mkataba wa kwanza kumalizika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI iliwasiliana na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na kuwaombea kibali cha ajira ambapo yalitolewa maelekezo kuwa Wahasibu Wasaidizi hawa waajiriwe na Halmashauri kwa mikataba na walipwe kwa kutumia mapato ya ndani hadi hapo Serikali itakapokuwa imewaajiri. Aidha, wahasibu hawa wana jukumu la kuhudumia Kituo husika na Zahanati zake zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haijaajiri wataalam wa manunuzi kwa kuwa manunuzi mengi katika Vituo vya Afya yanafanywa na Pharmacists ambao wapo katika Vituo vyote vya kutolea huduma ikizingatiwa kuwa asilimia kubwa ya fedha kwa Vituo hivyo ni kwa ajili ya manunuzi ya dawa, vifaa vya tiba kupitia Bohari Kuu ya Dawa ya Serikali (MSD).

Serikali itaendelea kuajiri Wahasibu Wasaidizi kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.