Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 2 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 19 2019-11-06

Name

Omary Ahmad Badwel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bahi

Primary Question

MHE. OMARY A. BADWEL aliuliza:-

Kwa muda mrefu sasa baadhi ya wananchi wamekuwa wakinufaika na mradi wa TASAF ambao kwa kiasi umekuwa ukifanya vizuri, aidha mradi huu umefika vijiji vichache tu na vijiji vingine bado havijafikiwa na Serikali iliahidi kuwa vijiji vyote vitanufaika na mradi huu.

(a) Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya mradi wa TASAF kufikia vijiji vyote nchi nzima?

(b) Kumekuwa na utaratibu wa baadhi ya viongozi kukata fedha za walengwa wa TASAF moja kwa moja kwa kuwakatia bima, michango mbali mbali ya vijiji na kadhalika bila ridhaa yao. Je, Serikali inatoa kauli gani katika jambo hilo?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omary Ahmad Badwel Mbunge wa Bahi lenye maswali mawili kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ulipoanza mwaka 2013 uwezo wa fedha uliokuwepo ulitosheleza kufikia Vijiji/Mtaa/Shehia 9,986 ikiwa ni asilimia 70 ya Vijiji/Mitaa/Shehia zote nchini. Vijiji/Mitaa/Shehia ambavyo havijafikiwa ni 6,858.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshakamilisha hatua zote za maandalizi ya Kipindi cha Pili cha Mpango huu wa Kunusuru Kaya Maskini ambacho kinatarajia kuanza utekelezaji mwishoni mwa mwaka huu 2019 baada ya Serikali kupata fedha. Kipindi cha Pili ya Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kitatekelezwa kwenye Halmashauri zote 185 za Tanzania Bara na Wilaya zote za Zanzibar katika Vijiji/Mitaa na Shehia zote ikiwa ni pamoja na kufika kwenye Vijiji/Mitaa/ Shehia 6,858 ambavyo bado havijafikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ufafanuzi kuhusu matumizi ya fedha za walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini. Fedha hizi ambazo ni ruzuku zinatolewa ili kaya iweze kugharamia mahitaji ya msingi kama chakula, gharama za elimu na afya na kuwekeza kwa ajili ya kuanzisha miradi ya kuongeza kipato. Hivyo, ni maamuzi ya kaya husika kupanga matumizi ya fedha hizi ili mradi haziendi kwenye matumizi ambayo hayaisaidii kaya kujikwamua na umaskini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika baadhi ya maeneo, viongozi wa vijiji wanalazimisha kukatwa kwa ruzuku za walengwa ili kukatiwa bima ya afya au kulipia michango mbalimbali. Hii si sawa na haikubaliki. Napenda kusisitiza, lakini vilevile niagize, kwamba walengwa wasikatwe fedha zao moja kwa moja bali walipwe stahiki zao na iwapo kuna michango inayotakiwa kama ni kwa ajili ya shughuli za maendeleo ya kijiji basi michango hii itozwe kwa wananchi wote wa kijiji husika na siyo kukata moja kwa moja kutoka fedha za walengwa wa TASAF peke yao. Nimalizie kwa kusisitiza kwamba viongozi wote waliokuwa wanatoa amri ya kukata fedha za walengwa wa TASAF moja kwa moja bila ridhaa ya walengwa hao, waache kufanya hivyo mara moja, kwa kuwa huu siyo utaratibu na wala siyo sahihi na vinginevyo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilieleze Bunge lako Tukufu kwamba, baadhi ya halamshauri zilishawahi kufanya hivyo na Wakurugenzi waliagizwa warudishe fedha hizo na tayari wamesharudisha. Ahsante.