Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 1 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 4 2019-11-05

Name

Albert Ntabaliba Obama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Primary Question

MHE. ALBERT O. NTABALIBA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutumia Kituo cha Forodha Manyovu ili kupitisha mizigo kwenda Burundi kwa kiwango cha kutosha?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Albert Obama Ntabaliba, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Forodha Manyovu kinatoa huduma za forodha mpakani mwa Tanzania na Burundi katika Mkoa wa Kigoma. Kituo hicho kinatoa huduma kidogo ikilinganishwa na uwezo wake kwa sababu ya changamoto ya umbali wa transit route ya Dar-es-Salaam hadi Burundi kupitia Manyovu.

Mheshimiwa Spika, umbali wa transit route ya Dar-es- Salaam – Isaka – Nyakanazi hadi Manyovu ni kilometa 1457 wakati transit route ya Dar-es-Salaam – Isaka – Nyakanazi hadi Kabanga ni kilometa 1330. Tofauti ya umbali kati ya transit route ya Kabanga na Manyovu ni kilometa 127. Aidha, transit route ya Dar-es-Salaam – Manyoni – Tabora hadi Manyovu ni kilometa 1273, lakini route hii pia inakabiliwa na changamoto ya ubovu wa sehemu ya barabara ambayo haijajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto ya umbali wa transit route ya Dar-es-Salaam - Isaka – Nyakanazi - Manyovu pamoja na ubovu wa sehemu ya barabara ya transit route ya Dar-es-Salaam – Manyoni – Tabora - Manyovu wafanyabiashara wengi hutumia Kituo cha Forodha Kabanga ili kuokoa sehemu ya gharama ya usafiri na usafirishaji.

Aidha, pamoja na changamoto hizi, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Kituo cha Forodha Manyovu kimeunganishwa na Mfumo wa Forodha wa Uthaminishaji Mizigo wa TANCIS na kina uwezo wa kutoa huduma za kiforodha kwa wakati na kwa ufanisi wa hali ya juu. Vilevile, taasisi mbalimbali za Serikali ikiwemo Uhamiaji, Polisi na Wizara ya Kilimo zimeanzisha Ofisi katika kituo hicho kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma za kiforodha.

Mheshimiwa Spika, ni matarajio ya Serikali kwamba huduma za forodha katika Kituo cha Forodha Manyovu zitaimarika zaidi baada ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa vipande vya barabara ya Manyoni – Tabora – Uvinza; ujenzi wa barabara ya Kasulu – Manyovu na ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha Kimataifa, pamoja na mradi wa ukarabati wa Bandari ya Kigoma.