Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 108 2020-02-07

Name

Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Primary Question

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI aliuliza:-

Wananchi wa Vijiji vinavyounda Jumuiya za Hifadhi ya Wanyamapori waliopo Namtumbo miaka 14 iliyopita walikubaliana kuacha ardhi yao kwa shughuli za hifadhi na kwamba ardhi hiyo isitumike kwa makazi wala kilimo cha mazao ya kudumu isipokuwa mpunga pekee. Wananchi washiriki kutunza njia za asili za wanyama hususan tembo na walikubaliana kwamba mipaka ya ardhi husika ingepitiwa upya baada ya kupita miaka 10 kuanzia mwaka 1996 walipoingia makubaliano:-

(a) Je, kwa nini Serikali imekiuka makubaliano hayo na kuwakaribisha wafugaji kwenye maeneo ya wananchi yaliyokuwa yakitumika kwa kilimo cha mpunga?

(b) Je, ni lini Serikali italipa fidia wakulima ambao mashamba yao ya mpunga yameathiriwa na ng’ombe wanaochunga katika mashamba hayo?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edward Amandus Ngonyani, Mbunge wa Namtumbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uwepo wa Jumuiya za Hifadhi ya Wanyamapori katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo zilizoanzishwa kwa kushirikisha wananchi wenyewe na kutangazwa katika Gazeti la Serikali. Aidha, Serikali haijabadili matumizi ya ardhi hiyo na kuwapatia wafugaji isipokuwa wapo baadhi ya wafugaji waliovamia maeneo hayo bila kufuata taratibu. Serikali inaendelea kuwabaini na kuwaondoa wafugaji ambao wamevamia maeneo yasiyoruhusiwa na kuwapeleka katika maeneo yaliyotengwa rasmi kwa shughuli za ufugaji.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, wapo baadhi ya wakulima waliovamia na kufanya shughuli za kilimo katika eneo la Jumuiya za Hifadhi ya Wanyamapori kinyume na sheria. Hivyo, hakuna fidia itakayolipwa na Serikali kwa wakulima waliovamia na kufanya shughuli za kibinadamu katika maeneo yasiyoruhusiwa. Viongozi wa Mkoa na Wilaya wanaelekezwa kusimamia na kuhakikisha yanatengwa maeneo rasmi kwa ajili ya shughuli za ufugaji na kilimo kuepuka uvamizi wa hifadhi.