Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 30 2019-09-05

Name

John John Mnyika

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Kibamba

Primary Question

MHE. JOHN J. MNYIKA aliuliza:-

Tume ya Taifa ya Uchaguzi iliwahi kupewa jukumu la nyongeza la kusimamia kura ya maoni ya mabadiliko ya Katiba kwa Sheria iliyotungwa na Bunge kwa kutumia Ibara ya 74(6)(e) ya Katiba ya Nchi:-

(a) Je, ni kwa nini Ibara ya 74(6)(e) isitumike ili Uchaguzi wa Vitongoji, Vijiji na Mitaa wa Mwaka 2019 usimamiwe na Tume ya Taifa ya Uchaguzi badala ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI)?

(b) Je, ni kwa nini Serikali haijatekeleza makubaliano na Vyama ya mwaka 2014 ya kuwezesha Uchaguzi wa Vitongoji na Mitaa kutumia Daftari la Wapiga Kura lililoboreshwa badala ya Orodha ya Wakazi?

(c) Je, ni hatua gani Serikali imechukua kuhakikisha Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2019 unakuwa huru na wa haki?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa John John Mnyika Mbunge wa Kibamba lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi yaliyoainishwa katika Ibara ya 74(6) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kusimamia uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani na kutekeleza majukumu mengine yoyote kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge. Jukumu la kusimamia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa si miongoni mwa majukumu ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa mujibu wa Katiba isipokuwa ni jukumu la Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya), Sura ya 287 na Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji), Sura ya 288. Hivyo, masharti ya Ibara ya 74(6)(e) ya Katiba hutumika tu pale ambapo kuna Sheria iliyotungwa na Bunge inayoipatia Tume ya Taifa ya Uchaguzi majukumu mengine.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kueleza, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi haina Mamlaka ya kusimamia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Kutokana na msimamo huo wa Kikatiba uchaguzi wa Serikali za Mitaa hauwezi kutumia daftari la kudumu la wapiga kura kwa kuwa daftari hilo lipo chini ya usimamizi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa mujibu wa masharti ya Kifungu cha 12 cha Sheria ya Uchaguzi, Sura ya 343. Kwa msingi huo, makubaliano yoyote yaliyowahi kufanyika kuhusu matumizi ya daftari la kudumu la wapiga kura katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa yanapaswa kuzingatia masharti ya Kikatiba na sheria za nchi.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unakuwa huru na haki Serikali imeandaa Kanuni na Miongozo ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa za Mwaka 2019 ambazo zimezingatia maoni yaliyotolewa na wadau mbalimbali wa uchaguzi vikiwemo vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu Tanzania pamoja na asasi za kiraia.