Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 2 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 18 2019-09-04

Name

Nassor Suleiman Omar

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Ziwani

Primary Question

MHE. NASSOR SULEIMAN OMAR aliuliza:-

Utamaduni katika kila nchi ni utambulisho wa Taifa; na kwa kuwa kuna upotevu mkubwa wa utamaduni wa asili kwenye makabila yetu nchini:-

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kufufua utamaduni wa asili wa makabila yetu?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Suleiman Omar Mbunge wa Ziwani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali ni msimamizi na mratibu wa shughuli zote za utamaduni ikiwepo sera ya utamaduni na sheria zinazohusu utamaduni jamii ndio mmiliki wa utamaduni. Hivyo, nitumie fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge akiwemo muuliza swali, taasisi, asasi na mashirika ya jamii nzima ya watanzania kuwa mstari wa mbele katika kulinda utamaduni wetu na kufufua pale unapofifia. Wizara yangu inatambua na kupongeza mwamko mpya katika jamii wa kuhimiza na kuendeleza utamaduni wetu maeneo kadhaa nchini kwa mfano: Tamasha la ngoma ya utamaduni la Dkt. Tulia Traditional dance ambalo linafanyika katika Mkoa wa Mbeya. Tamasha la majimaji Serebuka Songea, Tamasha la Bulambo ambalo linafanyika Mwanza, Tamasha la Chamwino Dodoma, Tamasha la Nyasa na Matamasha ya makabila mbalimbali yanayoendelea katika Kijiji cha Makumbusho Jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Serikali wizara yangu mbali na kuhimiza matumizi ya lugha ya Kiswahili ndani na nje ya nchi inaendelea na tafiti za kiutamaduni za makabila mbalimbali nchini lengo likiwa ni kuhifadhi. Mkazo zaidi umewekwa kwenye tamaduni za makabila au jamii zenye wazungumzaji wachache ambao zipo katika hatari ya kutoweka. Aidha, wizara inashirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii katika kuendesha tamasha jipya la urithi wa utamaduni inasimamia kila mwaka tamasha la kimataifa ya sanaa na utamaduni Bagamoyo ambao ni kivutio kikubwa kwa wanasanaa, wadau wa sanaa na wapenzi wa sanaa kutoka ndani na nje ya nchi na kwa sasa wizara inaratibu tamasha la utamaduni wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (JAMAFEST) litarajiwa kufanyika Jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 21 hadi 28 mwezi mwaka na mwaka huu na kuwavutia wanasanaa na wadau takribani laki moja kutoka ndani na nje ya Jumuiya.