Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 25 2020-01-29

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-

Mwelekeo wa Serikali kwa sasa ni kuimarisha utalii wa picha badala ya utalii wa uwindaji kwenye Mapori yetu ya Akiba nchini: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwa na lango la utalii wa picha kwenye Pori la Akiba la Selous kwenye Ukanda wa Kusini kwenye Wilaya za Tunduru na Liwale?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohammed Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Niabu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imendelea na jitihada za kupanua wigo wa mazao ya utalii kulingana na rasilimali zilizopo. Mazao hayo ni pamoja na utalii wa uwindaji, utalii wa picha, utalii wa utamaduni na utalii wa fukwe na namna ambayo itanufaisha Taifa na Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa azma hiyo, tarehe 26 Julai, 2019, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Joseph Pombe Magufuli akiwa katika ziara yake ya kikazi kwenye uzinduzi wa Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa Nyerere, alitoa maelekezo kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kuwa sehemu ya Pori la Akiba Selous ipandishwe hadhi kwa kuanzisha Hifadhi Taifa Nyerere. Azimio la kuanzisha Hifadhi ya Taifa Nyerere lilipitishwa na Bunge lako Tukufu kwenye kikao cha tarehe 9 Septemba, 2019 na kuridhiwa na Mheshimiwa Rais kwa GN. No. 923 ya mwaka 2019. Kwa mujibu wa Sheria, shughuli za utalii zinazoruhusiwa kwenye hifadhi za Taifa ni zile za kuangalia na kupiga picha tu na uwindaji hauruhusiwi.

Mheshimiwa Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kuwa, kufuatia kuanzishwa kwa Hifadhi ya Taifa Nyerere, Wilaya za Tunduru na Liwale ni miongoni mwa wilaya zitakazonufaika na fursa za moja kwa moja za utalii wa picha katika maeneo hayo. Aidha, tathmini itafanyika ili kuona sehemu ya kuweka lango la kuingilia katika Hifadhi ya Taifa ya Nyerere itaweza kuwekwa kuendeleza utalii.