Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 1 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 5 2020-01-28

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Primary Question

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:-

Wilaya ya Rufiji ni moja ya Wilaya kongwe nchini na inakadiriwa kuwa na watu takribani 350,000; eneo la Wilaya ni kubwa na huwalazimu wananchi kusafiri umbali wa kilometa 100 kufuata huduma za kibenki.

Je, ni lini Serikali itapeleka huduma za kibenki katika Wilaya ya Rufiji?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa upatikanaji wa huduma za kifedha na hasa karibu na maeneo ya wananchi ili kuwawezesha kuendesha shughuli zao za kiuchumi. Aidha, kufuatia mabadiliko ya sekta ya fedha nchini ya mwaka 1991 Serikali ilitoa uhuru kwa mabenki kufanya tathimini na utafiti ili kuamua kuhusu maeneo ya kupeleka huduma za kibenki kulingana na taarifa za utafiti uliofanywa pamoja na vigezo vya benki husika. Kwa kuwa benki zinajiendesha kibiashara maamuzi ya kufungua tawi sehemu yoyote hapa nchini huzingatia vigezo hivyo.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Wilaya ya Rufiji wanapata huduma za kifedha kupitia kituo cha makusanyo ya fedha cha NMB yaani cash collection point kilichopo Kata ya Utete pamoja na mawakala wa benki hususan Benki ya NMB na CRDB waliopo katika Wilaya ya Rufiji.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Mbunge wa Rufiji aendelee kuwahimiza wananchi wake kutumia fursa zilizopo za kupata huduma za kifedha kupitia kituo hicho cha makusanyo ya fedha cha NMB, mawakala wa benki na simu za mkononi wakati Serikali ikiendelea kufanya jitihada za kuboresha miundombinu muhimu pamoja na kufanya majadiliano na kuyashawishi baadhi ya mabenki ili kuona jinsi ya kupunguza baadhi ya vikwazo vinavyoweza kusababisha gharama za uendeshaji wa shughuli za kibenki katika Wilaya ya Rufiji kuwa juu.