Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 27 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 228 2019-05-14

Name

Dr. Immaculate Sware Semesi

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI aliuliza:-

Ibara ya 13(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema kwamba “Watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria”; lakini kumekuwa na kiwango cha juu cha matukio na kesi zinazohusu kuvunjwa kwa haki za kiraia kwa kufanywa na vyombo vya dola:-

(a) Je, kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015 ni kesi ngapi zimefunguliwa Mahakamani kuhusu madhara yanayofanywa na vyombo vya dola dhidi ya raia, na huchukua muda gani hadi kutolewa hukumu?

(b) Je, kesi hizo zimekuwa zikigharamiwa kwa kiasi gani kutoka Mfuko wa Fedha za Umma tangu mwaka 2010 – 2015?

(c) Je, Serikali inafanya jitihada gani kuhakikisha wananchi wake pamoja na vyombo vya usalama wanapata elimu ya uraia?

Name

Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware Semesi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015 Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora haijafungua kesi yoyote Mahakamani kuhusu madhara yanayofanywa na vyombo vya dola dhidi ya raia. Tume imekuwa ikipokea malalamiko ya uvunjwaji wa haki za binadamu dhidi ya vyombo vya dola na kuyashughulikia kwa kufanya uchunguzi wa kawaida, usikilizwaji hadharani na kufanya usuluhishi na upatanishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbinu hizi zimeonekana kuwa na mafanikio makubwa katika kuwapatia wananchi haki yao wanayostahili, hivyo kutokuwa na umuhimu wa kufungua mashauri Mahakamani. Ikumbukwe kuwa ufunguaji wa mashauri Mahakamani ni hatua ya mwisho iwapo njia nyingine zote zimeshindikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeeleza, kwa kuwa Tume haijawahi kufungua kesi yoyote ya haki za binadamu katika Mahakama zetu kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015, hivyo basi, hakuna gharama zozote za ufunguaji wa mashauri Mahakamani zinazohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi cha mwaka 2010 – 2015, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imefanya jitihada mbalimbali ili kuhakikisha wananchi pamoja na vyombo vya usalama wanapata elimu ya uraia. Jitihada hizo ni pamoja na kuelimisha Umma kupitia vyombo mbalimbali vya habari, mikutano, maadhimisho, machapisho na warsha mbalimbali katika kipindi cha 2010 hadi 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla ya vipeperushi na vijitabu 40,638, makala 18,300 za Mpango Kazi wa Kitaifa wa Haki za Binadamu, majarida yaliyowekwa kwenye tovuti ya Tume ni matano, vipindi vya redio na televisheni ni 115 na kufanya mikutano na wananchi kuhusu haki za binadamu na hasa katika kumiliki ardhi kwenye mikoa 21 ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata katika kipindi cha kuanzia 2015 hadi sasa, jitihada hizi zimeendelea kufanywa na Wizara yangu Waheshimiwa Wabunge na Bunge hili kwa ujumla kwamba haki zitakuwa zinatendeka na kwamba tunaendelea kubuni mbinu na mikakati mbalimbali itakayowezesha kuendelea kuwafikia wananchi wengi iwezekanavyo.