Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 14 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 118 2016-05-06

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA aliuliza:-
Matukio ya kubakwa na ulawiti kwa watoto nchini yamekuwa yakijirudia mara kwa mara na watuhumiwa walio wengi huachiwa au humalizana na wazazi wa waathirika kifamilia:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa kesi hizo hazimalizwi kifamilia?
(b) Je, ni mkakati gani umewekwa ili kuhakikisha kuwa watuhumiwa hao wanapopatikana na hatia wapewe adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine wenye nia mbaya?
(c) Je, watoto waliopatwa na matukio hayo wamewekewa mazingira gani ili kuwaondoshea msongo wa mawazo na kuendelea na elimu bila kubughudhiwa na wenzao.

Name

Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Agelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b), na (c), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli matukio ya kubakwa na kulawitiwa, watoto yamekuwa yakitokea na kuripotiwa katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Pia ni kweli kuwa baadhi ya kesi za aina hiyo zimekuwa zikimalizwa kifamilia kwa maridhiano kati ya mtuhumiwa na wazazi wa mtoto muathirika. Hivyo kuwapa shida sana Wapelelezi wa kesi hizo kupata ushahidi.
(a) Tatizo la kuficha ushahidi na kuzimaliza kesi hizo kifamillia haliwezi kumalizwa na Vyombo vya Dola vinavyofanya uchunguzi peke yake bila ushirikiano na wananchi wanaoishi na watuhumiwa. Hivyo, Serikali imekuwa ikitoa elimu kwa umma kwa kuficha ushahidi na kuyamaliza matukio hayo ati kifamilia siyo kosa la jinai peke yake, bali vile vile, utaratibu huo unachochea vitendo hivyo kuendelea katika jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ili kuweka mazingira rafiki kwa waathirika na wananchi wenye taarifa au ushahidi wa aina hiyo, Serikali imeanzisha madawati ya jinsia katika vituo mbalimbali vya Polisi yanayopokea taarifa kutoka kwa wananchi na kuliwezesha Jeshi la Polisi kuendesha upelelezi kwa ufanisi. Pindi tukio la kubaka au kulawiti linaporipotiwa upelelezi hufanyika na mtuhumiwa hufunguliwa mashtaka mara moja. Kwa utaratibu huu Serikali inahakikisha kuwa matukio haya hayamalizwi nje ya utaratibu wa haki jinai.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako Tukufu tumetunga sheria zenye adhabu kali kwa watuhumiwa wa makosa hayo, wanapopatikana na hatia. Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16, imeweka adhabu ya kifungo cha maisha kwa mtu yeyote anayekutwa na hatia ya kumbaka msichana, hicho ni Kifungu cha 136(1) au miaka 14 kwa anayekutwa na hatia ya kujaribu kumbaka msichana, Kifungu cha 136(2). Pia sheria imeweka adhabu ya kifungo cha miaka 14, kwa kosa la kulawiti Kifungu cha 154.
Mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kuwa, sheria hizi zinasimamiwa ipasavyo na kuendelea kuimarisha upelelezi na uendeshaji wa mashauri ya ubakaji na ulawiti ili kuiwezesha Mahakama kutoa adhabu stahiki pindi mtuhumiwa anapopatika na hatia.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, waathirika wa vitendo hivi viovu, hupata msongo wa mawazo na kujisikia vibaya mbele ya wenzao, hali ambayo ina athari mbaya kwenye masomo yao na makuzi ya watoto hao. Serikali imeanza utekelezaji wa mwongozo wa mwaka 2015 wa kuzuia ukatili dhidi ya watoto, mwongozo ambao unataka Walimu Washauri, wateuliwe kila shule ya Msingi na Sekondari na kupatiwa mafunzo ya ushauri nasaha.