Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 27 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 222 2019-05-14

Name

Ester Alexander Mahawe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. MAHAWE Aliuliza:-

Halmashauri ya Mbulu haina Hospitali ya Wilaya hivyo wananchi wa Kata za Gidhim, Yayeda, Ampatumat hutembea umbali mrefu kufuata huduma katika kituo cha Afya Dongobeshi.

(a) Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi Kituo cha Afya Dongobesh ili kiweze kuwahudumia wananchi wa Mbulu Vijijini na kupunguza msongamano katika Hospitali ya Rufaa ya Hydom?

(b) Je, ni lini Serikali itaongeza Watumishi wa Afya, dawa na vifaa tiba katika kituo hicho cha afya?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Ester Mahawe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwe Mwenyekiti, Kituo cha Afya Dongobeshi kilianzishwa mnamo mwaka 1974 kipo kata ya Dongobeshi, kinahudumia jumla ya wakazi takribani 30,000 wa Tarafa ya Dongobeshi na wakazi wa maeneo jirani wakiwemo wananchi wa Kata za Gidhim, Yaeda na Amputamat.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa kituo hiki, Serikali kwa nyakati tofauti imekuwa ikitoa fedha kwa lengo la kuboresha miundombinu pamoja na huduma za afya zitolewazo kwenye kituo hiki. Mwezi Machi, 2018 Serikali ilitoa kiasi cha shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa majengo ambayo ujenzi wake umekamilika hivi karibuni. Majengo hayo ni wodi ya Mama na Mtoto (Maternity and Pediatric Ward), jengo la upasuaji, jengo la maabara, nyumba moja ya mtumishi na jengo la kuhifadhia maiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuongeza idadi ya watumishi katika Kituo cha Afya cha Dongobeshi. Mwaka wa fedha 2017/2018 watumishi sita wapya wameajiriwa na kufanya kituo kuwa na jumla ya watumishi 37. Aidha, Serikali imetuma fedha bohari Kuu ya Dawa (MSD) jumla ya shilingi milioni 320 zikiwa ni kwa ajili ya kunua vifaa tiba, hadi sasa vifaa vyenye thamani ya shilingi milioni 37 vimepelekwa kituoni hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa fedha 2018/2019, jumla ya shilingi bilioni 1.5 zimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu inayojengwa katika Tarafa ya Dongobesh. Kukamilika kwa hospitali hii kutaondoa msongamano kwenye Hospitali ya Hydom. Kwa kuwa, Hospitali ya Wilaya inajengwa katika eneo la Dongobesh hakuna sababu ya Kituo cha Afya kilichopo sasa kupandishwa hadhi kuwa hospitali.