Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 27 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 220 2019-05-14

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-

Moja kati ya vigezo vya “Capital Development Grant Assessment”ni namna Halmashauri inavyoweza kutoa taarifa kwa wananchi juu ya mtiririko wa fedha ambazo Serikali imepeleka katika Halmashauri na miradi iliyokusudiwa kutekelezwa:-

(a) Je, kwa nini mchakato huo ulisitishwa?

(b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kurejesha mchakato huo ambao utakuwa ukiongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali nchini?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremia Komanya, Mbunge wa wa viti Maalum lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, upimaji wa Halmashauri ulikuwa ni kigezo cha kuziwezesha Halmashauri kupata ruzuku ya maendeleo isiyo na masharti (Local Government Development Grant) kuanzia mwaka 2005. Miongoni mwa vigezo vilivyozingatiwa ni kuwepo kwa uwazi katika mapokezi na matumizi ya fedha kwenye ngazi ya Vijiji, Kata na Mitaa kwa kuhakikisha mapato na matumizi yanabandikwa kwenye mbao za matangazo. Mradi huo ulitekelezwa kupitia fedha za wafadhili ambapo Serikali pia ilikuwa na mchango katika fedha hizo. Mradi huo ulifikia ukomo mwaka 2013, baada ya wafadhali kujitoa na Serikali kuendelea kutekeleza mradi huo kuanzia mwaka 2014/2015 na 2017/2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutoa ruzuku ya maendeleo kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuziwezesha kutekeleza miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwemo afya na elimu. Wananchi wanachangia nguvu kazi na vifaa mbalimbali kwa ajili ya ukamilishaji wa miradi hiyo. Serikali inakubaliana na wazo la kuzipima Halmashauri katika matumizi ya ruzuku hiyo inayotolewa na Serikali kwenye Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hilo liko kwenye mjadala ndani ya Serikali ili kuona namna bora ya kulitekeleza katika kuhakikisha kunakuwa na uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya fedha zinazotolewa na Serikali kwenye Halmashauri hadi ngazi ya vijiji.