Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 26 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 211 2019-05-13

Name

Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-

Fedha za kuchochea Maendeleo ya Jimbo (CDCF), zimekuwa msaada mkubwa katika kusaidia Maendeleo Majimboni.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza viwango vya fedha hizi ili kuleta ufanisi zaidi?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge Konde kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo yaani Constituency Development Catalyst Fund, ulianzishwa kwa Sheria ya Bunge Namba 16 ya Mwaka 2009 yaani The Constituency Development Catalyst Fund Act, 2009. Lengo la Mfuko ni kuhakikisha miradi ambayo ni vipaumbele vya wananchi katika Jimbo husika na ambayo haikupata fedha katika bajeti inapata fedha za utekelezaji. Kwa tafsiri ya Sheria iliyoanzisha Mfuko, fedha za Jimbo ni kwa ajili ya Majimbo ya uchaguzi ambayo yameanzishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuzingatia Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungao wa Tanzania. Vigezo vinavyotumika kugawa fedha ni ukubwa wa eneo, idadi ya watu na kiwango cha umasikini katika Jimbo husika.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikiongeza fedha hizi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha ambapo mwaka 2018/ 2019, Serikali iliongeza kiasi kinachotolewa kutoka shilingi bilioni 10 zilizokuwa zikitolewa kipindi cha nyuma mpaka shilingi bilioni 12.5 na Serikali itaendelea kuongeza kiwango cha fedha kinachotolewa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutumia fedha za Mfuko wa Jimbo umeainishwa katika Sheria ya Mfuko Kifungu Na. 10(1) kwamba kutakuwa na Kamati ya Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo katika kila halmashauri ambayo Mwenyekiti wake ni Mbunge wa Jimbo husika. Miongoni mwa majukumu ya msingi ya Kamati hii ni kuchambua miradi inayowasilishwa kutoka kwenye jamii na kuidhinisha miradi itayotekelezwa na jukumu la Mkurugenzi Mtendaji ni kusimamia utekelezaji wa maamuzi ya Kamati hii. Ahsante.