Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 21 Industries and Trade Wizara ya Viwanda , Biashara na Uwekezaji 169 2019-05-06

Name

Deogratias Francis Ngalawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Primary Question

MHE. EDWIN M. SANNDA (K.n.y. MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA) aliuliza:-

Serikali iliahidi kulipa fidia wananchi walioachia maeneo yao kupisha miradi ya makaa ya mawe, Mchuchuma na Liganga lakini mpaka sasa hawajalipwa:-

(a) Je, ni lini Serikali italipa fidia hizo ili wananchi husika waendelee na shughuli nyingine za kiuchumi?

(b) Je, kwa nini Serikali haitoi mrejesho pindi panapotokea mkwamo?

(c) Je, Serikali inaweza kuthibitisha kuwa miradi hiyo itaanza kutekelezwa kama ilivyoahidi Bungeni?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya uthamanishaji mali ya wananchi watakaopisha mradi unganishi wa Mchuchuma na Liganga awamu ya kwanza ilikamilika tarehe 18 Agosti, 2015, lakini ulipaji fidia kwa wakati huo haukuweza kufanywa. Kwa vile muda mrefu ulikuwa umepita, Serikali ilifanya uhakiki na uthaminishaji mwingine mwezi Desemba, 2018 ambapo imebainisha malipo stahiki yatakayopaswa kulipwa. Taratibu hizo zimekuwa shirikishi na zikifanywa kwa kuwahusisha Mamlaka husika ikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa katika maeneo ya miradi. Malipo ya fidia kwa mujibu wa uthaminishaji wa sasa utafanywa pindi taratibu za msingi za kimaandalizi zikikamilishwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi huo umeanza kutekelezwa kwa kufanya maandalizi ya awali ambapo pamoja na mambo mengine yanajumuisha upembuzi yakinifu wa mradi, uthaminishaji wa mali na maeneo ya wananchi watakaopisha mradi na kujenga barabara ya kiwango cha changarawe kuunganisha eneo la mradi na barabara kuu ya lami li kuwezesha kufikisha mitambo na huduma nyingine katika eneo la mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizo kasi ya utekelezaji imekuwa ndogo kutokana na changamoto mbalimbali zilizojitokeza hususan majadiliano na mwekezaji kuchukua muda mrefu zaidi kuliko tulivyotegemea. Hata hivyo, Serikali inaendelea kuangalia njia bora zaidi ya kuwezesha mradi huo kuendelea kutekelezwa kwa tija na kuleta manufaa mapana zaidi kwa wananchi wa eneo hilo na Taifa letu kwa ujumla.