Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 19 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 155 2019-05-02

Name

Yosepher Ferdinand Komba

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. YOSEPHER F. KOMBA aliuliza:-

Kuna uhaba wa watumishi na vitendea kazi katika Idara ya Ardhi na Maliasili – Wilaya ya Muheza kunakosababisha kuazima watumishi na vifaa kutoka Halmashauri nyingine:-

(a) Je, ni lini Serikali itaajiri watumishi na kununua vitendea kazi katika Idara hiyo?

(b) Je, Serikali iko tayari kuwawekea wananchi Wanasheria ili kusaidia kutatua migogoro ya ardhi?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yosepher Ferdinand Komba, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Idara ya Ardhi na Maliasili katika Halmashauri ya Wilaya ya Muheza inao watumishi 12 kati ya 20 wanaohitajika. Halmashauri imeendelea kuomba vibali kwa ajili ya kuajiri watumishi hao. Hata hivyo,ili kukabiliana na upungufu huo Halmashauri imeajiri watumishi watatu (3) wa Ardhi kwa mkataba ili kutatua changamoto mbalimbali za ardhi. Vile vile katika mwaka wa fedha 2017/2018, kupitia mapato yake ya ndani Halmashauri ilinunua GPS- RTK (Real time Kinematic) kwa ajili ya upimaji ardhi kwa gharama ya shilingi milioni 37. Aidha, Halmashauri imetoa gari Toyota Land Cruiserkwa ajili ya Idara ya Ardhi na Maliasili. Halmashauri itaendelea kununua vitendea kazi kwa awamu kadri ya upatikanaji wa Fedha.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inao mfumo wa kisheria wa utatuzi wa Migogoro ya Ardhi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ambao umeainishwa katika Sheria ya Utatuzi wa Migogoro ya Ardhi, Na. 2 ya mwaka 2002 na Kanuni zake. Migogoro ya ardhi iliyopo Wilayani Muheza imegawanyika kwenye makundi makuu matatu; migogoro ya kiwilaya ambayo inahusisha mipaka ya vijiji vya Wilaya ya Muheza na Tanga Jiji pamoja na Vijiji vya Muheza na Pangani. Migogoro hii inashughlikiwa katika ngazi ya Mkoa na itapatiwa ufumbuzi wakati wowote.

Kundi la pili la migogoro ni migogoro ya mipaka ya vijiji iliyotokana na zoezi la upimaji wa mipaka nchi nzima uliofanyika mwaka 2007. Vikao kwa ajili ya kumaliza migogoro hii vinaendelea na vimefikiwa hatua nzuri. Migogoro mingine ni migogoro ya viwanja ambayo hupokelewa na kutatuliwa kwa utaratibu wa kawaida wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. Suluhisho la kudumu kwa aina hii ya migogoro ni kukamilisha mpango wa matumizi bora ya ardhi, kupima viwanja na kurasimisha makazi ambapo mpaka sasa makazi 4,768 yamerasimishwa Wilayani Muheza. Serikali itaendelea kutekeleza Mpango waMatumizi Bora ya Ardhi, kurasimisha makazi, kupima viwanja na mashamba ili kumaliza migogoro ya ardhi.