Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 18 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 150 2019-04-30

Name

Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Primary Question

MHE. JANET Z. MBENE aliuliza:-

Serikali ilinunua mashine ya kujengea kutoka Marekani kwa fedha nyingi sana kwa lengo la kuitumia kujenga nyumba nyingi za watumishi, ofisi na taasisi na kadhalika kwa haraka zaidi, mashine hiyo kwa muundo wake ina uwezo wa kujenga nyumba kwa bei nafuu zaidi na hivi sasa kuna upungufu mkubwa wa nyumba za walimu, madarasa, maabara, mabweni, nyumba za wauguzi, madaktari na vituo vya afya:-

(a) Je, ni nyumba ngapi na kwa gharama gani zilizojengwa na Jeshi la Ulinzi na Kujenga Taifa kwa kutumia mashine hiyo na kama zimejengwa kwa ujenzi wa kawaida zingetumia kiasi gani?

(b) Je, ni kwa nini mashine hiyo haitumiki kujenga nyumba zinazohitajika wakati kuna upungufu mkubwa sana wa nyumba za Serikali?

(c) Je, Serikali iko tayari kufanya tathimini na kutuletea Bungeni mpango mzima wa kuanza kutumia mashine hiyo kujenga nyumba zinazohitajika?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI (K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Janet Zebedayo Mbene, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba nne zilijengwa wakati wa mafunzo kwa gharama ya shilingi 1,325,000,000 na majengo matano yalijengwa baada ya mafunzo kwa gharama ya shilingi 9,216,653,699.50. Gharama za majengo yote jumla yake ilikuwa ni shilingi 10,541,653,699.50. Majengo haya ni pamoja na ukumbi (multipurpose hall) na nyumba za kuishi katika Kambi ya Twalipo Dar es Salaam; Banda la Jeshi la Wananchi wa Tanzania la Maonesho Sabasaba; na Ofisi ya muda ya Kitengo cha Uwekezaji TIC. Nyingine ni Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Kihangaiko; Kiteule cha Kijeshi Tarime; Karakana ya Wakala wa Vipimo na Mizani Misugusugu Kibaha; ghala la kuhifadhia nafaka la SUMA JKT kule Chita; na kumbi za burudani za SUMA JKT Mwenge Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo haya kama yangejengwa kwa ujenzi wa kawaida gharama zingefikia shilingi 11,981,649,808.70. Mbali na teknolojia hii kuwa ya nafuu katika gharama za ujenzi uliofikia asilimia 15%, unafuu mkubwa upo katika ujenzi unaokadiriwa kuwa na asilimia 70%.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwango kikubwa mashine hizi hazitumiki ipasavyo kutokana na ukosefu wa fedha za maendeleo kwa ajili ya ujenzi wa substructure yaani ujenzi toka chini hadi usawa wa msingi. Malighafi inayotumka ni steel coil ambayo kwa matumizi ya Kijeshi kama fedha za maendeleo zingepatikana ingeweza kukidhi mahitaji.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, mitambo ya UBM (Ultimate Building Machine) ilinunuliwa na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa ajili ya kutekeleza shughuli za ujenzi ndani za Wizara. Hata hivyo, Wizara ya Ujenzi na Jeshi la Kujenga Taifa liko tayari kushirikiana pamoja na taasisi nyingine za Serikali katika ujenzi wa majengo hayo. Aidha, Wizara iko tayari kuandaa mpango kabambe kwa kutumia teknolojia hiyo ili kuwezesha ujenzi wa majengo mbalimbali ya Serikali. Ahsante.