Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 17 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 144 2019-04-29

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

Kuna taarifa kwamba nchi ya Kenya inatarajia kutekeleza mpango wa kujenga mabwawa makubwa kwa ajili ya uzalishaji umeme. Kwa kuwa ujenzi huo unatishia ustawi wa uwepo wa Hifadhi ya Taifa Serengeti. Je, Serikali ya Tanzania inachukua hatua gani kuhusu mpango huo?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maluum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Serikali ilipata taarifa ya mpango wa ujenzi wa mabwawa ya umeme uliopangwa kutekelezwa na Serikali ya Kenya. Wizara ilifanya uchunguzi wa madhara yatakayosababishwa na miradi hiyo katika Hifadhi ya Taifa Serengeti kwa kukusanya takwimu za mtiririko wa maji na kulinganisha na mahitaji halisi ya miradi iliyotarajiwa. Uchunguzi ulibaini kuwa utekelezaji wa miradi hiyo, ungesababisha athari kubwa ya kiikolojia ya Serengeti kwani takwimu zilizotumiwa na wataalam wa nchini Kenya kuhalalisha mradi huo hazikuwa sahihi. Miongoni mwa athari hizo ni pamoja na kuhatarisha ustawi wa maisha ya viumbe hai kutokana na ukosefu wa maji katika Mto Mara wakati wa kiangazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya Mto Mara yanajadiliwa na Tume ya kuratibu Bonde la Ziwa Victoria (Lake Victoria Basin Commission) chini ya Wizara ya Mambo Nchi za Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Aidha, majadiliano mbalimbali kuhusu hatima ya Mto Mara au miradi inayoathiri maji ya Mto Mara ikiwemo ujenzi wa Bwawa la Umeme la Ewaso, Ngiro nchini Kenya yanaendelea kujadiliwa katika mpango wa Bonde la Mto Mara uliosainiwa mwezi Septemba, 2016 chini ya Wizara ya Maji. Katika pango huo suala la athari za ujenzi mabwawa kwa maliasili zitakazoathirika kutokana miradi itakayofanyika nchini Kenya na Tanzania limejadiliwa na mapendekezo kutolewa kuhusu namna ya kukabiliana na matumizi yenye utata.