Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 17 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 138 2019-04-29

Name

Maria Ndilla Kangoye

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIA N. KANGOYE aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya vituo vya Afya Mkoani Mwanza kukosa vyumba vya upasuaji:-

Je, ni nini mpango wa Serikali wa kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi kwa kucheleweshwa kufanyiwa upasuaji?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maria Ndilla Kangoye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza una jumla vya vituo vya kutolea huduma za Afya vya Serikali 272 ikiwepo Hospitali sita, Vituo vya Afya 35 na Zahanati 231. Kwa sasa huduma ya upasuaji wa dharura kwa akina mama inatolewa kwenye Hospitali zote sita na Vituo 10 vya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupunguza vifo vinavyotokana na uchelewashwaji wa akina mama wakati wa kujifungua kwa kutokufanyiwa upasuaji, mwaka wa fedha 2017/2018 na 2018/2019 Serikali imepeleka kiasi cha shilingi bilioni sita kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa Vituo vya Afya 14 Mkoani Mwanza ambavyo kwa sasa viko katika hatua ya ukamilishaji na hivyo kuna Vituo 11 vya Afya ambavyo vilikuwa havitoi huduma za upasuaji, vitaanza kutoa huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali ilipeleka kiasi cha shilingi bilioni tatu Mkoani Mwanza kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya za Ilemela na Buchosa ambazo zitatoa huduma ya upasuaji wa dharura kwa akina mama, hivyo kutanua wigo na kuboresha huduma za upasuaji Mkoani Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kujenga vituo vya kutolea huduma za afya na kuongeza wataalam ili kumaliza tatizo la vifo vya akina mama vinavyotokana na uchelewashaji wa huduma ya upasuaji wakati wa kujifungua.