Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 7 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 56 2019-04-10

Name

Muhammed Amour Muhammed

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Bumbwini

Primary Question

MHE. MUHAMMED AMOUR MUHAMMED aliuliza:-

Suala la mafuta ni la Muungano na kumekuwepo na taratibu mbalimbali zinazofanywa ili kutafuta mafuta nchini:-

Je, ni taratibu zipi zilizopaswa kufanyika ili kuthibitisha kwamba mafuta yanapatikana katika eneo husika?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Muhammed Amour Muhammed, Mbunge wa Bumbwini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa mujibu wa Katiba iliyopo, suala la utafutaji na uzalishaji mafuta ghafi ni suala la Muungano. Hata hivyo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar mwaka 2015 kwa nia njema ya kuongeza ufanisi na tija katika shughuli za kutafuta na kuzalishaji mafuta ghafi, zilikubaliana kuwa kila upande usimamie shughuli hizo kwa kutumia sheria na taasisi zake. Serikali zetu za pande zote mbili za Muungano zimefanya hivyo katika masuala ya bandari na viwanja vya ndege, pamoja na kuwa masuala hayo ni ya Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuthibitisha mafuta yanapatikana katika eneo husika, taratibu zifuatazo hufanyika ikiwa ni pamoja na:

(a) Utafiti wa awali wa kukusanya sampuli za kijiolojia na kijiochemia;

(b) Kukusanya data za kijiofizikia (gravimetry na seismic);

(c) Kufanya tathmini (interpretation) ya data za kijiolojia na kijiofizikia;

(d) Kutambua maeneo ya mashapo (geological structures) katika miamba tabaka ambapo mafuta au gesi inaweza kukusanyika kufuatia matokeo ya tathmini ya data za kijiolojia na kijiofizikia; na

(e) Kuchimba visima vya utafiti (exploration wells) katika maeneo yalikotambulika mashapo ili kuthibitisha uwepo wa mafuta ghafi au gesi asilia.