Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 45 2019-04-09

Name

Jesca David Kishoa

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. JESCA D. KISHOA) aliuliza:-

Kwa muda mrefu sasa Mkuu wa Wilaya ya Ikingu amekuwa akijichukulia sheria mkononi na kuwanyanyasa wananchi wa Kata za Ighombwe, Iglansoni na maeneo ya Wilaya ya Ikungi.

Je, Serikali inaweza kutoa majibu ni mamlaka yapi aliyonayo Mkuu huyo wa Wilaya ya kuwanyanyasa na kuamrisha mali za wananchi kuchomwa moto au kuporwa na Serikali bila utaratibu wowote wa kisheria kwa kisingizio kuwa wanaishi maeneo yasiyoidhinishwa kwa makazi?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Igombwe, Iglasoni na maeneo ya Wilaya ya Ikungi zinapakana na hifadhi ya Msitu wa Minyughe yenye ukubwa wa hekta 264,600. Kwa nyakati tofauti shughuli za kibinadamu kwenye vijiji vinavyozunguka msitu huu zilianza kuhatarisha mazingira ya hifadhi hasa baada ya wananchi kadhaa kuhamia eneo la hifadhi na kujenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kupitia vikao vya kisheria vya Baraza la Madiwani liliazimia kuulinda msitu huu na kuwaondoa wavamizi, hivyo Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ambayo ndiyo yenye mamlaka aliyopewa na Sheria ya Tawala za Mikoa ya Regional Administrative Act ya mwaka 2002, chini ya Kifungu cha 15 kutoa amri halali, iliwataka wananchi hao kuondoka katika maeneo ya Hifadhi ya Msitu wa Minyughe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la kuwaondoa wavamizi lilifanyika kwa awamu mbili, yaani Mei na Oktoba, 2017 ambapo watu 119 waliondolewa kwenye hifadhi hiyo pamoja na ng’ombe 2,243, mbuzi 455 na kondoo 169. Zoezi hili lilishirikisha Askari wa Jeshi la Polisi waliofanya kazi yao kwa weledi wa hali ya juu kwa sababu hakuna raia aliyejeruhiwa wala kupoteza mali zake. Ni dhahiri uwepo wa Askari Polisi ambao ni wasimamizi wa sheria uliwezesha operesheni hiyo kufanyika salama na hakuna kielelezo wala ushahidi kwamba haki zao za msingi zilivunjwa.