Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 5 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 33 2019-04-08

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE.DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-

Katika Ilani ya CCM kuhusu huduma za afya nchini ni kujenga zahanati katika vijiji na kituo cha afya katika kila kata; kwa sasa Jimbo la Igunga lina vituo vya afya viwili tu katika kata 2 kati ya 17 na zahanati kwenye vijiji 19 tu kati ya vijiji 68:-

(a) Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya kwenye kata 15 zilizosalia?

(b) Je, ni lini Serikali itajenga zahanati kwenye vijiji 49 vilivyosalia?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa NaibuSpika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 kwa ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya kote nchini kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo. Halmashauri ya Wilaya ya Igunga ilipokea shilingi milioni 800 kwa mwaka wa fedha 2018 kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya vya Igurubi na Simbo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Kituo cha Afya cha Simbo ambacho ujenzi wake upo asilimia 97, fedha hizo zilitumika kumalizia majengo mawili ambayo ni jengo la upasuaji, nyumba ya mtumishi pamoja na ujenzi wa majengo mapya manne ambayo ni maabara, jengo la uzazi, jengo la kufulia na jengo kuhifadhi maiti. Aidha, kituo hicho kimeanza kupokea vifaa tiba kutoka Bohari Kuu ya Dawa (MSD). Kwa upande wa Kituo cha Afya Igurubi, ujenzi unaendelea na umefikia asilimia 70. Jumla ya majengo manne mapya yamejengwa ambayo ni maabara, jengo la uzazi, jengo la kufulia na jengo la kuhifadhi maiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutekeleza ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya kwa awamu katika Halmashauri ya Wilaya ya Igunga kulingana na upatikanaji wa rasilimali fedha. Ahsante.