Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 2 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 16 2019-04-03

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Primary Question

MHE. DAVID E. SILINDE aliuliza:-

Katika kipindi cha hivi karibuni wananchi wamekuwa wakilalamikia mzunguko wa fedha kuwa mdogo:-

Je, hali hiyo imesababishwa na nani?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania inatekeleza Sera ya Fedha inayolenga kusimamia mzunguko wa fedha unaoendeana na mahitaji halisi ya uchumi kwa lengo la kudumisha utulivu wa mfumuko wa bei na hivyo kuweka mazingira mazuri ya ukuaji wa uchumi.

Mheshimiwa Spika, kabla ya mwaka 2017 kulitokea changamoto ya kuongezeka kwa mikopo chechefu ambayo kwa sehemu kubwa ilisababishwa na baadhi ya taasisi za fedha kutoa mikopo bila kuzingatia Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 na Kanuni zake za mwaka 2008. Ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali ilichukua hatua ya kusimamia kwa karibu Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 pamoja na Kanuni zake ikiwa ni pamoja na kuhamisha fedha za taasisi za umma kutoka kwenye mabenki ya biashara kwenda Benki Kuu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kufuatia hali hiyo, kuanzia Januari, 2017, Serikali kupitia Benki Kuu ilichukua hatua za kuongeza ukwasi kwenye uchumi ili kutatua changamoto ya kupungua kwa mzunguko wa fedha katika soko. Hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kushusha riba ya Benki Kuu (discount rate) kutoka asilimia 16 Machi, 2017 hadi asilimia 7 Agosti, 2018. Pili, Benki Kuu ilipunguza kiwango cha kisheria cha sehemu amana kinachotakiwa kuwekwa Benki Kuu na mabenki ya biashara (Statutory Miminimum Reserve Requirement, SMR) kutoka asilimia 10 hadi asilimia 8 mwezi Aprili, 2017. Tatu, kuruhusu mabenki kutumia asilimia 10.0 ya sehemu ya SMR kama chanzo kimojawapo cha kusaidia hali ya ukwasi kwenye uchumi. Mwisho, Benki Kuu ilianzisha utaratibu wa kutoa mikopo ya muda maalumu kwa mabenki pamoja na kununua fedha za kigeni kutoka kwenye soko la jumla la mabenki ili kuongeza ukwasi kwenye uchumi.

Pili, Benki Kuu ilipunguza kiwango cha kisheria cha sehemu ya amana kinachotakiwa kuwekwa Benki Kuu na Benki ya Biashara (Statutory Minimum Reserve Requirement) kutoka 10% hadi 8% mwezi Aprili, 2017.

Tatu, kuruhusu mabenki kutumia 10% ya sehemu ya Statutory Minimum Reserve Requirement kama chanzo kimojawapo cha kusaidia hali ya ukwasi katika uchumi.

Mwisho, Benki Kuu ilianzisha utaratibu wa kutoa mikopo ya muda maalum kwa mabenki pamoja na kununua fedha za kigeni kutoka kwenye soko la jumla la mabenki ili kuongeza ukwasi kwenye uchumi.

Mheshimiwa Spika, hatua hizi za Sera ya Fedha zimesaidia kuboresha hali ya ukwasi kwenye Benki za Biashara na kupunguza riba katika Soko la Fedha baina ya mabenki kutoka wastani wa asilimia 4.6 kwa mwaka unaoishia Februari, 2018 hadi asilimia 2.3 kwa mwaka unaoishia Februari, 2019. Kuongeza kwa mikopo ya sekta binafsi kutoka wastani wa asilimia 1.7 mwaka 2017 hadi asilimia 7.3 Januari, 2019 na kupungua kwa riba ya mikopo kutoka wastani wa asilimia 21 mwaka 2016 hadi wastani wa asilimia 17 mwaka 2018.

Hivyo basi, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba kwa sasa hakuna tatizo la mzunguko mdogo wa fedha katika soko baada ya Serikali kuchukua hatua hizi. Pia mzunguko wa fedha katika uchumi unaendana na malengo na mahitaji halisi ya shughuli za kiuchumi zilizopo.