Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 4 2019-04-02

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-

Kulikuwa na mgogoro wa mipaka kati ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti (SENAPA) na vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo; wananchi wa vijiji hivyo walienda mahakamani na wakaishinda TANAPA kwa sababu mipaka iliyokuwa iwewekwa na TANAPA haikuwa shirikishi na haikufuata GN iliyoanzisha SENAPA:-

(a) Je, ni lini Serikali itapitia upya mipaka hiyo kwa kushirikisha vijiji husika na kuzingatia GN iliyoanzisha SENAPA?

(b) GN iliyoanzisha IKorongo Game Reserve inatofautiana na mipaka iliyowekwa; je, ni lini marekebisho yatafanyika ili iendane na GN?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, migogoro ya mipaka kati ya hifadhi ya Taifa ya Serengeti na baadhi ya vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo haujatatuliwa kwa kuwa yapo madai ya Rufaa ya Ardhi Namba 256 ya mwaka 2018 katika Mahakama Kuu ya Jiji la Mwanza dhidi ya hukumu iliyotolewa na mahakama. Utatuzi wa mgogoro huo unasubiri matokeo ya rufaa iliyowasilishwa Mahakama Kuu dhidi ya hukumu iliyotolewa awali. Baada ya maamuzi ya mahakama kutolewa, Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na vijiji husika itapitia upya mipaka kati ya hifadhi na vijiji kwa kuzingatia maamuzi ya mahakama.

(b) Mheshimiwa Spika, Pori la Akiba la Ikorongo lilianzishwa kisheria kwa GN 214 ya tarehe 10 Juni, 1994. Hapo awali pori hilo lilikuwa likisimamiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti ambayo iliweka alama za mipaka ya pori hilo mwaka 2000 kwa kuzingatia GN husika. Aidha, kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wananchi wa Kijiji cha Park Nyigoti yaliyoifikia Wizara yangu, kuwa sehemu ya eneo la kijiji hicho lipo ndani ya Pori la Ikorongo.

Mheshimiwa Spika, kufuatia kuwepo kwa malalamiko hayo, Wizara itashirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya uhakiki wa mipaka katika maeneo ya hifadhi yenye malalamiko ikiwemo kijiji cha Park Nyigoti ambacho kinapakana na Pori la Akiba Ikorongo.