Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 10 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 118 2019-02-08

Name

Sabreena Hamza Sungura

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. SABREENA H. SUNGURA) aliuliza:-

Michezo ni afya, furaha, burudani, undugu na pia huondoa au kupunguza uhalifu nchini. Kuwa na viwanja vyenye hadhi kama kile cha Jakaya Kikwete Youth Park huvutia vijana wengi nchini kupenda michezo:-

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga viwanja vyenye hadhi hiyo nchi nzima?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ujenzi wa viwanja vya michezo nchini si suala la Serikali peke yake bali jamii nzima ya Watanzania zikiwemo taasisi za umma, asasi za kiraia na kampuni za watu binafsi. Wajibu wa Serikali ni kuonesha njia kwa ujenzi mkubwa wa viwanja changamani kama vile Uwanja wa Taifa na Uwanja wa Uhuru ulioko Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, viwanja vyote viwili sasa hivi viko katika ukarabati mkubwa utakaogharimu zaidi ya shilingi bilioni tatu ili kujiweka tayari kwa Mashindano ya Mpira wa Miguu wa Bara la Afrika kwa watoto chini ya umri wa miaka 17 yatakayofanyika mwezi wa Nne mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ukarabati huo mkubwa Serikali imekamilisha maandalizi yote ya awali na ya kiufundi ikiwemo upatikanaji wa eneo la hati miliki, uwekaji wa mipaka ya eneo lote pamoja na beacons, ununuzi wa gari mbili za mradi huo, tathmini ya kimazingira, tafiti za eneo, upembuzi yakinifu wa mradi na michoro ya ubunifu wa ujenzi wa uwanja huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kiwanja cha Jakaya Mrisho Kikwete Youth Park cha Dar es Salaam anachokiongelea Mheshimiwa Mbunge kimejengwa kutokana na mahusiano ya karibu kati ya Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Ilala chini ya Mbunge wake Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu na Kampuni ya Symbion kwa kushirikiana na Club ya Sanderland.

MWENYEKITI: Hampigi makofi? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo kama ni kuonesha njia Serikali imeshafanyika hivyo na itaendelea kujenga viwanja vingine kadiri mahitaji yatakavyojitokeza na uwezo wa kifedha utakavyopatikana.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kulipongeza Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) kwa uboreshaji wa Viwanja vya Kaitaba Kagera, Nyamagana Mwanza, na Mikoa ya Iringa, Singida na Lindi kwa kuonyesha njia katika upatikanaji wa viwanja bora vya michezo nchini.