Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 10 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 111 2019-02-08

Name

Naghenjwa Livingstone Kaboyoka

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RUTH H. MOLLEL (K.n.y. MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA) aliuliza:-

SUMA-JKT Idara ya Zana za Kilimo ilikopesha 5,355,153,000/= kwa idara mbalimbali ndani ya SUMA-JKT. Taarifa za CAG zimeonesha kuwa hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2016 ni kiasi cha Sh.534,785,000/= ambayo ni kiasi chini ya asilimia 10 ndio kilirejeshwa:-

(a) Je, ni kiasi gani hadi sasa kimerejeshwa kwenye Idara hiyo ya Zana za Kilimo?

(b) Je, Serikali itakubaliana na mimi kwamba, uzembe huu wa kutohakikisha mikopo ya fedha za Serikali inarudishwa kwa wakati ili wakulima wengine nao waweze kukopeshwa kumechangia kukwamisha juhudi za kupunguza umaskini nchini?

(c) Je, Serikali inachukua hatua gani kuwawajibisha waliohusika na utoaji huo wa mikopo bila kuhakikisha inarudishwa kwa wakati?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye Sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa mradi wa zana za kilimo wa SUMA-JKT ulikopesha miradi mingine ndani ya SUMA-JKT jumla ya shilingi 5,355,153,000/= kama ilivyoelezwa katika Taarifa ya CAG ya mwaka 2015/2016 na kwamba mpaka kufikia tarehe 30 Juni, 2016, kiasi cha shilingi 534,785,000/= ndicho kilikuwa kimerejeshwa. Hadi kufikia tarehe 31 Januari, 2019, jumla ya shilingi 2,389,082,000/= zimerejeshwa katika mradi wa zana za kilimo ambayo ni sawa na asilimia 45 ya fedha zote zilizokopeshwa. Hivyo, mpaka sasa fedha ambazo bado hazijarejeshwa ni shilingi 2,966,071,000/=.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kubwa la kukopesha fedha hizo lilikuwa ni kuiwezesha kimtaji miradi ndani ya SUMA-JKT pamoja na miradi mingine mipya baada ya kujiridhisha kuwa ina tija. Hivyo, lengo hili halikwamishi juhudi za kupunguza umasikini nchini, basi linaongeza mapato katika miradi ya shirika kwa ujumla.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la SUMA-JKT limeendelea kuhakikisha fedha zilizobaki zinarejeshwa katika mradi wa zana za kilimo kwa kuchukua hatua zifuatazo:-

(i) Kuhakikisha uwepo wa mikataba kati ya mradi wa zana za kilimo na mkopaji, pia mikataba iliyokuwa na upungufu imerekebishwa;

(ii) Kuhakikisha miradi iliyokopeshwa inazalisha kwa faida ambapo sehemu ya fedha hiyo huwasilishwa moja kwa moja katika mradi wa zana za kilimo; na

(iii) Kuweka baadhi ya miradi iliyokopeshwa chini ya usimamizi wa moja kwa moja wa mradi wa zana za kilimo.