Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 session 13 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 15 2018-11-07

Name

Catherine Nyakao Ruge

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CATHERINE N. RUGE aliuliza:-
Bado kuna kata ambazo hazina shule za sekondari hivyo kufanya baadhi ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kwenda na kurudi shuleni, kutokana na hali hiyo baadhi ya wazazi wameamua kuwapangishia vyumba watoto wao mitaani kwenye mazingira ambayo si salama.
Je, kwa nini Serikali isije na mpango mahususi wa ujenzi wa mabweni kama inavyofanya kwenye madawati ili kuwapunguzia wanafunzi hasa wa kike adha ya kutembea umbali mrefu kwenda na kurudi nyumbani?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI napenda kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Nyakao Ruge, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inamiliki na kuendesha shule za sekondari 3,634 Tanzania Bara. Kati ya hizo shule 3,519 ni za kutwa na shule 155 ni za bweni. Idadi hiyo ukiilinganisha na kata 4,420 inabainisha kuwepo na kata ambazo hazina shule za sekondari hivyo zipo changamoto za baadhi ya wanafunzi kutembea umbali mrefu kufuata shule kwenye kata za jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pendekezo la Mheshimiwa Mbunge la kujenga mabweni katika shule zote sekondari kuwa zuri, Serikali imeweka kipaumbele kujenga mabweni kwanza kwenye shule za kidato cha tano na sita pamoja na zinazoandaliwa kupandishwa hadhi kuwa za kidato cha tano na sita ambazo husajili wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi. Tangu mwaka 2014 Serikali imetumia shilingi bilioni 29.4 kujenga mabweni 298 kwenye shule za sekondari na mabweni 25 kwenye shule za msingi.
Aidha, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imepanga kutumia jumla ya shilingi bilioni 15.7 kujenga mabweni 206 katika shule za sekondari na mabweni manne katika shule za msingi. Halmashauri zinahimizwa kuendelea kushirikiana na wananchi na wadau wengine kujenga shule za sekondari kwenye kata ambazo hazina shule na kujenga dahania (hostel) kwenye shule za sekondari zenye wanafunzi wanaotembea umbali mrefu.