Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 session 13 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 09 2018-11-06

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Mwaka 2017 wakati Mheshimiwa Rais akiwa katika ziara Mkoa wa Kigoma, katika Wilaya ya Kasulu aliwaruhusu wananchi waliokuwa wakilima katika maeneo ya Hifadhi ya Makere (Kagera Nkanda) kwa sharti kwamba wasiongeze maeneo mengine zaidi ya yale waliyokuwa wakilima:-
Je, kwa nini TFS wanapingana na agizo la Mheshimiwa Rais na wanawatesa wananchi kwa kuwapiga na kuwanyan’ganya baiskeli na pikipiki?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, baada ya Mheshimiwa Rais kuagiza kumegwa kwa sehemu ya msitu wa Makene Kusini ili kutoa maeneo kwa wananchi kulima Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kasulu ilitekeleza agizo kikamilifu kwa kupima eneo la msitu huo.
Mheshimiwa Spika, kufuatia upimaji huo jumla ya hekta 10,012.61 zilitengwa kwa ajili ya kilimo kwa wananchi wa maeneo hayo. Hivyo Kijiji cha Uvinza kilipewa hekta 2,174 na Kagera Nkanda kikapewa hekta 2,496; na eneo lingine la hekta 5,342.61 zilitengwa kwa ajili ya wananchi wengine wa vijiji vya Nachenda, Mgombe na Nyakitonto.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kijiji cha Uvinza kililalamika kuwa eneo walilopata halitoshi hivyo wakaomba waongezewe eneo ambalo ni ardhi chepechepe yaani ardhi oevu karibu na Mto Makene na Mto Malagarasi ambalo kitaalam hairuhusiwi kulima kwa sababu itasababisha uharibifu mkubwa na kupotea kwa sifa ya uhifadhi. Mto Malagarasi ni muhimu kwa ikolojia na kwa ajili ya ujenzi wa mitambo ya umeme wa maji katika maporomoko ya Mto Malagarasi.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa wananchi wanaendelea na shughuli za kilimo katika maeneo hayo yaliyotengwa na kuridhiwa na vikao vyote vya Mabaraza ya Mkoa na Wilaya. Wizara kwa kushirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa imekamilisha mchakato wa ramani mpya ya msitu huo.
Mheshimiwa Spika, tatizo lililojitokeza sasa ni kwa wananchi wachache kwa maslahi yao kukataa kufuata taratibu na kutaka kulima ndani ya msitu nje ya maeneo yaliyotengwa huku wengine wakiendelea na uwindaji haramu wa wanyamapori. Wananchi hao wasiofuata sheria ndio waliozuiwa na mamlaka husika kwa Sheria ya Misitu namba 14 ya mwaka 2002, Sura 323 katika kifungu cha 26 ambacho kinakataza kufanya shughuli zozote za kibinadamu ikiwa ni pamoja na kilimo na ufugaji ndani ya msitu wa hifadhi. Mtu yoyote akibainika kufanya hivyo hatua za kisheria hufuatwa.
Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa wananchi kuendelea na kilimo katika maeneo yaliyotengwa na kuachana na kilimo cha kuhamahama ambacho ndicho kinachowafanya kuvamia maeneo ya hifadhi za misitu. Aidha, natoa ushauri kwa wananchi kufuata kanuni bora za kilimo kwa kutumia mbolea ili mashamba yao yaendelee kuzalisha mazao wakati wowote.