Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 6 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 66 2019-02-04

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. AIDA J. KHENANI) aliuliza:-

Kumekuwa na utaratibu wa Serikali kuchukua maeneo kwa wananchi na kuahidi kuwalipa, lakini huchukua muda mrefu kuwalipa.

Je, Serikali haioni kuwa kufanya hivyo ni kuwanyima wananchi haki yao ya msingi?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ulipaji wa fidia hufanyika kwa mujibu wa Sheria Namba 4 ya mwaka 1999 na Sheria Namba 5 ya mwaka 1999. Sheria hizi zinaelekeza kwamba pindi Serikali au mamlaka nyingine inapotwaa maeneo ya wananchi, wanatakiwa kulipa fidia stahiki, kamili na kwa wakati. Pamoja na Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999 Serikali ilitunga Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini Namba 7 ya mwaka 2016 ambayo imeelekeza kuwa pindi uthamini unapofanyika waliothaminiwa mali zao wanapswa kulipwa ndani ya miezi sita. Baada ya miezi sita tozo yaani prevailing interest rate in commercial banks inapaswa kuongezwa kwenye malipo ya madai ya fidia husika. Aidha, baada ya kupita kwa kipindi cha miaka miwili toka uthamini wa awali ufanyike, sheria inaelekeza pia, uthamini wa eneo hilo utafanyika upya.

Mheshimiwa Spika, licha ya taratibu za ulipaji wa fidia kuwekwa wazi katika sheria, kumekuwepo na malalamiko kutoka kwa wananchi katika maeneo mbalimbali kuhusu ucheleweshaji wa malipo ya fidia. Katika kutatua changamoto hizo Wizara imeandaa mwongozo unaozitaka taasisi zote zinazotaka kuchukua mali za wananchi kuwasilisha uthibitisho wa uwezo wa kulipa fidia kabla ya kuidhinishiwa kwa taarifa za uthamini wa mali unaotarajiwa kuchukuliwa. Aidha, mwaka 2016 Wizara ilizindua Mfuko wa Fidia ya Ardhi utakaosaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikijitokeza katika ulipaji wa fidia. Mfuko huo umepewa jukumu la kuratibu malalmiko ya ulipaji fidia na kusimamia malipo yote ya fidia yanayofanywa na watu au taasisi binafsi, ili kuhakikisha kuwa viwango vinavyotumika ni vile vilivyokubaliwa kwa wakati huo.

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kuwa changamoto ya ucheleweshaji wa malipo ya fidia imepatiwa ufumbuzi kwa kiasi kikubwa. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa changamoto hii inafikia mwisho ili kuondoa usumbufu usio wa lazima kwa wananchi.