Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 12 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 103 2016-05-04

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. HUSSEIN M. BASHE (K.n.y. MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU) aliuliza:-
Kifungu na 97(1)(b) cha Sheria ya Madini ya mwaka 2010 kinamtaka mwekezaji kabla hujaanza shughuli za kujenga mgodi ili kuzalisha madini ni lazima ahakikishe kwamba anawasilisha na kutekeleza mpango wa fidia, ujenzi wa makazi mapya na kuwahamishia wananchi waliopisha ujenzi huo kwenye makazi mapya yaani “compensation, reallocation and resettlement plan” kulingana na matakwa ya Sheria ya Ardhi.
Je, ni lini Serikali itarekebisha Sheria ya Ardhi ili iendane na matakwa ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali Namba103 la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ardhi yenye madini pamoja na kutawaliwa na Sheria ya Madini Na. 14 ya mwaka 2010 pia hutambuliwa na Sheria mama za sekta ya ardhi. Kwa kutambua hilo, kifungu cha 4(1) cha Sheria ya Madini kinatoa tafsiri ya mmiliki halali wa ardhi (lawful occupier) kuwa ni mtu ambaye anamiliki ardhi chini ya Sheria ya Ardhi Na. 4 na 5 za mwaka 1999. Hivyo, ni wajibu wa wamiliki wa migodi kuhakikisha kwamba wanatekeleza masharti ya Sheria ya Madini na Sheria ya Ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Ardhi Na. 4 na 5 za mwaka 1999 kifungu cha 3(1)(f) vinabainisha kwamba ardhi ina thamani na kwamba thamani hiyo inazingatiwa wakati wowote katika mapatano yoyote yanayoathiri maslahi hayo. Sheria hizi zinasisitiza kwamba lazima ardhi ilipwe fidia kamili kwa bei ya soko, haki na kwa wakati kwa yeyote ambaye ardhi yake imetwaliwa. Aidha, katika Kanuni za Sheria ya Ardhi Na. 4 ya mwaka 1999, Kanuni ya 10 ya “The Land (Compensation Claims) Regulations” ya mwaka 2001, inaelekeza kuwa fidia lazima iwe ya fedha lakini Serikali inaweza kutoa fidia katika muundo wa kitu kimoja kati ya hivi au vyote kwa pamoja:-
(a) Kiwanja kinacholingana na kile kilichotwaliwa;
(b) Jengo au majengo yanayolingana na yale yaliyotwaliwa;
(c) Mimea au mbegu; na
(d) Kutoa nafaka na vyakula vya msingi kwa wakati maalum.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Ardhi Na. 4 ya mwaka 1999, imezingatia matakwa ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010. Hivyo, kwa sasa hakuna sababu ya kufanya marekebisho ya Sheria ya Ardhi ili iendane na Sheria ya Madini katika suala la ulipaji wa fidia.