Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 4 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 50 2019-02-01

Name

Halima Abdallah Bulembo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO (K.n.y MHE. HALIMA A. BULEMBO) aliuliza:-

Kagera ni moja ya mikoa mitano maskini zaidi nchini kutokana na utafiti uliofanywa na Bwana Joachim De Weeidt na kuchapishwa kwenye jarida la Journal of Development Studies ambao unaonyesha kuwa kuna njia mbili za kuondoa umaskini Kagera ambazo ni kilimo na biashara:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwa na miradi maalum ya kuondoa umaskini kwa watu wa Kagera ambao ndiyo mkoa pekee unaopakana na nchi nyingi zaidi za EAC na hivyo kuufanya kuwa Mkoa wa kimkakati kibiashara?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Abdallah Bulembo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yote ya kiuchumi na kijamii inayotekelezwa na Serikali pamoja na sekta binafsi katika Mkoa wa Kagera na mikoa mingine nchini ni kwa ajili ya kuondoa umaskini na kuboresha maisha ya wananchi. Pamoja na ukweli huo, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba mkakati wa Serikali wa kutekeleza miradi maalum ya kuondoa umaskini katika Mkoa wa Kagera imeainishwa kwenye Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/2017 – 2020/2021, Mpango Mkakati wa Mpango wa Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo na Mipango ya Mkoa wa Kagera kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya mikakati inayoendelea kutekelezwa na kuratibiwa na Serikali katika Mkoa wa Kagera ni kama ifuatavyo:-

(i) Mkoa wa Kagera umeainisha na kutenga maeneo ya uwekezaji yenye ukubwa wa hekta 58,000 kwa ajili ya kuanzisha viwanda vya kusindika na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo (Agro Processing Industries), hususan viwanda vya kusindika nyama, ngozi, maziwa, asali, ndizi, miwa, kahawa, samaki na kadhalika. Aidha, hekta 17,400 kati ya hekta 58,000 zimeshapimwa na zipo tayari kwa uwekezaji.

(ii) Kukuza sekta ya viwanda, hususan viwanda vya kusindika mazao ya maliasili na kilimo. Viwanda vinavyofanya kazi ya kusindika mazao kwa sasa ni Kagera Fish Company Ltd na Supreme Perch Ltd vinavyosindika minofu ya samaki; Kagera Sugar Company Ltd na Amir Hamza Company Ltd vinavyosindika miwa na kahawa; na Kiwanda cha Maziwa kinachosindika wine ya rosella na juisi. Aidha, Kampuni ya Josam imepatiwa eneo lenye ukubwa wa hekta 500 katika Ranchi ya Kikulula na tayari limejengwa bwawa kwa ajili ya kuvuna maji pamoja na kuanza ufugaji wa ng’ombe wa maziwa wapatao mia moja hadi sasa.

(iii) Kuimarisha miundombinu ya barabara kwa kiwango cha lami mfano barabara ya Kyaka - Bugene (Km 59.1); barabara ya Kagoma – Lusahunga (Km 154); barabara ya Ushirombo – Lusahunga (Km 110); barabara ya Bwanga – Kalebezo (Km 67); barabara ya Nyakanazi – Kibondo (Km 50) na ujenzi umefikia asilimia 40; na barabara ya Kyamyorwa – Buzirayombo (Km 120).

(iv) Kuanzisha Kiwanda cha Kuchakata madini ya bati katika Wilaya ya Kyerwa ifikapo Juni 2021. Kampuni ya Tanzaplus Minerals and African Top Minerals Ltd zimeonesha nia ya kuwekeza na tayari zimeanza kuleta mashine za uchenjuaji.

(v) Kuendeleza mradi wa Uwekezaji wa Madini ya Nikeli Kabanga, katika Wilaya ya Ngara ifikapo Juni, 2021.

(vi) Kukamilisha Mradi wa REA Phase III katika maeneo ambayo hayajapata umeme ifikapo mwaka 2020.

(vii) Kuanzisha na kuendeleza skimu ya umwagiliaji katika eneo la Kitengule, Wilaya ya Karagwe ifikapo mwaka 2021. Ujenzi wa daraja la kuunganisha eneo la mradi na Kiwanda cha Sukari Kagera unaendelea kwa sasa. Wakulima zaidi ya 2,000 wanatarajiwa kunufaika na uwekezaji huo.

(viii) Kukamilisha ujenzi wa mtambo wa kufua umeme wa MW 80 kutoka Mto Rusumo na Kakono MW 87 katika Mto Kagera ifikapo Juni 2020.

(ix) Kuimarisha usafiri wa majini kwa kukamilisha ujenzi wa meli kubwa itakayotoa huduma ya usafiri na usafirishaji kati ya Bukoba na Mwanza.