Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 1 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 9 2019-01-29

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Kwa kuwa msimu wa pamba wa mwaka 2018/2019 ulikuwa na bei elekezi ndogo ya Sh.1,100 na kwa kuwa mara nyingi bei hizo elekezi zinapendekezwa kwa msukumo wa bei ya pamba duniani:-

(a) Je, Serikali katika msimu wa mwaka 2019/2020 ina mkakati gani wa kuinua bei ya wakulima kutoka Sh.1,100 hadi Sh.2,500?

(b) Kwa kuwa kuna Vyama vya Ushirika na Benki ya Wakulima, je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza tatizo la usambazaji wa mbegu za pamba katika Wilaya ya Bunda na hasa Jimbo la Bunda ambapo kila mwaka kunakuwa na uhaba wa mbegu na kutofika kwa wakati?

Name

Innocent Lugha Bashungwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karagwe

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, bei za mazao na bidhaa mbalimbali hutegemea nguvu ya soko kwa kuzingatia kiwango cha uzalishaji (supply), mahitaji (demand), ubora na viwango vinavyohitajika katika masoko ya ndani na nje na ushindani uliopo katika masoko husika.

Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa bei ya pamba kutoka Sh.1,100 hadi Sh.2,500 katika msimu wa ununuzi wa 2019/2020 kutategemea nguvu za soko hususani kupanda kwa bei ya pamba katika soko la dunia. Aidha, pamoja na kutegemea nguvu ya soko la dunia, Serikali inatekeleza mikakati ya kuhamasisha uwekezaji katika Viwanda vya Nyuzi na Nguo ili kuimarisha soko la ndani na ushindani.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imechukua hatua ya kuongeza upatikanaji wa mbegu za pamba nchini, ambapo katika msimu wa mwaka 2018/2019 jumla ya tani 27,851 zilizalishwa na kusambazwa kwa wakulima ikilinganishwa na tani 20,496 zilizozalishwa msimu wa mwaka 2017/2018 ikiwa ni ongezeko la asilimia 36. Aidha, kati ya mbegu zilizozalishwa mwaka 2018/2019, tani 1,075 zimesambazwa katika Wilaya ya Bunda ikilinganishwa na tani 688 zilizotumika msimu wa kilimo wa mwaka 2017/2018 ikiwa ni ongezeko la asilimia 56.

Mheshimiwa Spika, Benki ya Maendeleo ya Kilimo inahudumia sekta ya kilimo kwa ujumla wake kwa kutoa mikopo yenye riba nafuu ukilinganisha na benki zingine. Aidha, Benki ya Kilimo inatarajia kushiriki katika ununuzi wa pamba sambaba na benki nyingine zilizopo nchini kwa kutoa mikopo kwa kampuni zitakazoshiriki katika ununuzi wa pamba kama ilivyofanyika msimu wa ununuzi wa mwaka 2018/2019.