Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 61 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 517 2018-06-29

Name

Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. JOSEPH L. HAULE aliuliza:-
Kumekuwa na migogoro ya mipaka kati ya hifadhi na wananchi kwenye vijiji vinavyopakana na Hifadhi hizo kama vile Ruhembe, Kitete, Kikwalaza, Mji Mpya, Ihambwe, Mululu na sasa Kitongoji cha Lugawilo, Kata ya Uleling’ombe:-
Je, ni lini Serikali itaweka mipaka ili wananchi hao wasiendelee kunyang’anjywa ardhi yao kwa kisingizio cha kuwa wameingia kwenye Hifadhi?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hakuna mgogoro wa mpaka kati ya Hifadhi ya Taifa Mikumi na Vijiji vya Ruhembe na Ihambwe wala na Vitongoji vya Kikwalaza na Mji mpya ambavyo vimepakana na Hifadhi ya Taifa Mikumi. Mgogoro uliokuwepo ulishughulikiwa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kilosa, Viongozi wa Hifadhi, Viongozi wa Vijiji na wajumbe wane kutoka kila kijiji. Uhakiki wa mpaka wakati wa usuluhishi wa migogoro hiyo ulisimamiwa na viongozi wa Ardhi wa Mji Mdogo Mikumi, wataalam wa Ardhi Wilaya ya Kilosa, Mshauri wa Ardhi Mkoa wa Morogoro na wataalamu wa mipaka wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Kufuatia utatuzi huo, eneo la mpaka unaotenganisha vijiji na hifadhi, ulifwekwa na vigingi vya kudumu (beacons) kuwekwa pamoja na vibao vya kuonesha mpaka wa hifadhi katika baadhi ya maeneo. Vilevile hifadhi imeendelea kusafisha mpaka wake na vijiji vyote kila Mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi ya Mikumi haina mgogoro wa mpaka na Kijiji cha Kitete Msindazi, kwani mpaka uliobainishwa na Tangazo la Serikali Na.121 la mwaka 1975 ulitafsiriwa ardhini kwa usahihi na wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambapo uliridhiwa na pande zote husika zilishirikishwa katika uhakiki wa mpaka huo ambao ni viongozi wa vijiji na Hifadhi ya Mikumi chini ya usimamizi ya Kamati ya Ulinzi wa Usalama ya Wilaya ya Kilosa. Hata hivyo, lipo eneo la ardhi (general land) ambalo siyo sehemu ya hifadhi wala kijiji kati ya mpaka wa hifadhi na Kijiji cha Kitete Msindazi. Kisheria eneo hilo liko chini wa Kamishna wa Ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna mgogoro wa mpaka kati ya Hifadhi ya Mikumi na Kitongoji cha Lugawilo, Kata ya Uleling’ombe kwa kuwa hifadhi haipakani na kijiji chochote cha Kata ya Uleling’ombe. Aidha, naomba Mheshimiwa Mbunge atakapopata nafasi atembelee Hifadhi ya Taifa Mikumi kupata uhalisia wa kile kinachofanyika.