Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 61 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 511 2018-06-29

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHANCE M. GETERE aliuliza:-
Mnamo tarehe 12 Januari, 2018 Jeshi la Polisi lilifanya msako mkali katika Kijiji cha Mekomario – Bunda na katika msako huo wananchi wa eneo hilo waliharibiwa mali zao kama ilivyothibitishwa na Mkuu wa Wilaya ya Bunda na kutangazwa kwenye vyombo vya habari yaani Star TV tarehe 15 Februari, 2018:-
Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya kulipa fidia wananchi kutokana na uharibifu huo?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ambaye anaongoza Wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa na Wilaya, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 12 Januari, 2018 zilienezwa tetesi katika Kijiji cha Mekomariro, Wilayani Bunda kwamba wezi kutoka katika Kijiji cha Remong’oroni, Wilayani Serengeti walikuwa wameiba mifugo ya wakazi wa Mekomariro. Badala ya kutoa taarifa Polisi ili wasaidiwe kitaalam kupitia uchunguzi wa Polisi kubaini walioibiwa na idadi ya mifugo iliyoibiwa, walijikusanya kwa utaratibu usiokubalika na kwenda katika Kijiji cha Remong’oroni, wakafanya vurugu zilizosababisha watu wawili wakazi wa Kijiji cha Remong’oroni kuuwawa kikatili na wakamteka mtoto mmoja wa kiume.
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa za ghasia hizo ziliporipotiwa Polisi, msako ulifanyika kuwabaini wahusika ambapo watuhumiwa nane wamefunguliwa mashtaka Mahakamani kwa kesi ya mauaji Na. RM 02/2018 ambayo bado inaendelea. Msako uliofanyika pamoja na ule wa watuhumiwa wengine waliojificha unaoendelea haujasababisha uharibifu wa mali za wananchi wa Mekomariro wala wa Remong’oroni. Kwa kuwa kesi inaendelea, nashauri tusubiri uamuzi wa Mahakama ili tupate ufumbuzi wa kisheria wa suala hilo.