Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 56 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 474 2018-06-22

Name

Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA aliuliza:-
Mkoa wa Tabora ni moja kati ya mikoa inayokabiliwa na tatizo kubwa la ndoa za utotoni na kusababisha watoto wengi wa kike kushindwa kumaliza elimu ya msingi au ya sekondari. Aidha, hivi karibuni Serikali ilikata rufaa juu ya ndoa za utotoni ikitaka iruhusiwe watoto wa kike kuolewa na umri kuanzia miaka 14 ambapo hii ni kinyume cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia watoto wa kike wa Mkoa wa Tabora angalau wengi waweze kwenda kupata elimu ya msingi na sekondari kwa kupunguza ndoa za utotoni?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa elimu kwa watoto wote wa kike na kiume wa Tanzania. Hii inadhihirishwa na uamuzi wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kuifanya elimu ya msingi na ya sekondari kuwa ni elimu ya lazima na kutolewa bila malipo. Lengo la mpango huu ni kuhakikisha watoto wetu wote ikiwa ni pamoja na watoto wa kike wanaipata elimu hiyo bila kikwazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia umuhimu wa elimu ya mtoto wa kike Serikali inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Elimu ambayo inalinda haki za mtoto kusoma hadi sekondari. Kupitia marekebisho yaliyofanywa kwenye Sheria ya Elimu na Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 2 ya mwaka 2016, ni marufuku kwa mtu yeyote na katika mazingira yoyote kuoana na msichana au mvualana anayesoma shule ya msingi au sekondari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni kosa kumpa mimba msichana anayesoma au sekondari na kwa yeyote anayesaidia msichana au mvulana anayesoma kuoa au kuolewa anakuwa ametenda kosa. Marekebisho haya yameweka adhabu kali kwa yeyote anayetenda makosa haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika kumlinda mtoto wa kike na ndoa za utotoni, licha ya Sheria ya Ndoa kuweka mazingira na vigezo vya mtoto wa kike kuolewa akiwa na miaka 15, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kuhakikisha mtoto huyu analindwa. Katika kulisimamia hilo, Serikali imeendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 ambayo pamoja mambo mengine imeainisha haki za mtoto ikiwemo haki ya kupata elimu na kutoa wajibu wa haki hizo kulindwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa ujumla kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuzuia vitendo vya kuwaozesha watoto wa kike. Si tu kwa mkoa wa Tabora bali katika nchi yote ili kuwawezesha watoto wetu wa kike kupata elimu ya msingi na sekondari na pale ambapo vitendo hivyo vinajitokeza wananchi wana wajibu wa kutoa taarifa na kushirikiana na vyombo vya Serikali ili kuhakikisha wanaofanya makosa hayo wanachukuliwa hatua za kisheria.