Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 56 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 471 2018-06-22

Name

Wilfred Muganyizi Lwakatare

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Bukoba Mjini

Primary Question

MHE. MICHAEL J. MKUNDI - (K.n.y MHE. WILFRED M. LWAKATARE) aliuliza:-
Kukua kwa elimu ya uraia na ufahamu wa mambo ya kisiasa kumefanya wananchi wengi kuupokea mfumo wa vyama vingi na kuchagua wawakilishi wengi wa Vyama vya Upinzani kuongoza Kamati za Maendeleo za Kata, Halmashauri za Miji, Miji Midogo, Wilaya, Manispaa, Majiji na Majimbo ya Ubunge na Udiwani:-
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kutengeneza kanuni, utaratibu na mfumo wa kutoa elimu na maelekezo kwa watendaji na viongozi wa Kiserikali kuyakubali na kupata ufahamu wa mabadiliko ya kisiasa yanayokua kwa kasi ili kuepusha migogoro na migongano ya usimamizi wa kazi baina ya watendaji wa Serikali na wawakilishi wa wananchi?
(b) Je, kwa nini Serikali isiweke utaratibu wa kuwa na uchaguzi huru na haki kama vile Tume Huru ya Uchaguzi na chombo huru cha kusimamia chaguzi za vitongoji, vijiji na mitaa?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kwanza uniruhusu nimsahihishe kidogo Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali kwa niaba, huyu Mheshimiwa haitwi Alfred Lwakatare anaitwa Wilfred Lwakatare. Naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Wilfred Lwakatare, Mbunge wa Bukoba Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, watendaji na viongozi wa Serikali wanafanya kazi kwa mujibu wa Katiba, Sheria, Kanuni, Taratibu na miongozo iliyopo. Ni wajibu wa viongozi na watumishi wote katika ngazi zote za Serikali kuzifahamu nyenzo hizo za kazi ili kuepusha migogoro na migongano baina yao. Serikali imekuwa ikiwaongezea uwezo wa kiutendaji na uongozi watendaji na viongozi wao kupitia mafunzo ya mara kwa mara na vikao vya kazi ili wawahudumie wananchi vizuri na kwa tija zaidi.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa, Mamlaka za Wilaya na Mamlaka za Miji, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa husimamia uchaguzi wa vitongoji, vijiji na mitaa ambao hufanyika ukiwa huru na haki kila baada ya miaka mitano kwa kushirikisha wadau wote wakiwemo viongozi wa vyama vya siasa ambao hutoa maoni yao kunzia kwenye maandalizi ya uchaguzi.