Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 54 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 459 2018-06-20

Name

Edwin Mgante Sannda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. EDWIN M. SANNDA aliuliza:-
Wananchi wa Vijiji vya Hurumbi, Dumi na Chandimo Kata ya Serya, Ausia, Mulua na Guluma (Suruke) pamoja na Hachwi, Kutumo na Chora (Kolo) katika Jimbo la Kondoa Mjini, kijiografia wana changamoto kubwa ya huduma muhimu za afya ambapo wanalazimika kufuata huduma hizo katika zahanati za jirani au hospitali ya mjini:-
Je, ni lini Serikali itatupatia Mobile Clinic kutatua changamoto hii?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Mgante Sannda, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Kondoa wanahitaji huduma za Hospitali Tembezi (Mobile Clinic) katika kuhakikisha wanapata huduma mbalimbali za kinga na tiba kwa urahisi. Hata hivyo, Serikali kupitia Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma imekuwa ikitoa huduma za Hospitali Tembezi katika Halmashauri zote za Mkoa kwa awamu.
Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa kuanzia tarehe 10 – 19 Agosti, 2017 Halmashauri ya Mji wa Kondoa, Chemba na Kondoa Vijijini kwa Kushirikiana na Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa ziliendesha huduma ya kibingwa kwa Hospitali Tembezi katika Hospitali ya Kondoa. Katika zoezi hili, jumla ya Madaktari Bingwa 31 walitoa huduma mbalimbali za kibingwa kwa wagonjwa 6,873 kwa mafanikio makubwa.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri kupitia Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mji imeanzisha huduma za Hospitali Tembezi kwa watu wanaoishi na VVU kila mwezi katika Zahanati za Kingale na Kolo ili kuwapunguzia wagonjwa adha ya kufuata huduma hii katika Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa itaendelea kutoa huduma hizi mara kwa mara kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa kupata huduma za kibingwa na huduma nyingine katika maeneo yao na kuepusha kuingia gharama kufuata huduma za kiafya.