Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 43 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 366 2018-06-04

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-
Kila mwaka wanyama waharibifu wamekuwa wanakula mazao ya wakulima katika Jimbo la Bunda na Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi katika kulipa fidia ya kifuta jasho na kifuta machozi kwa wakulima hao:-
Je, Serikali ina mikakati gani ya kuzuia wanyama hao wakiwemo Tembo?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wizara inatambua madhara yanayosababishwa na wanyamapori waharibifu na wakali, hususan tembo, kwa wananchi waishio kandokando ya maeneo ya hifadhi, ikiwemo Wilaya ya Bunda. Katika Wilaya ya Bunda Vijiji vinavyopata usumbufu wa mara kwa mara kutokana na wanyamapori waharibifu na wakali ni Kunzugu, Bukore, Nyatwali, Balili, Tamau, Serengeti, Nyamatoke, Kihumbu, Hunyari, Mariwanda, Mugeta, Guta, Kinyambwiga na Kinyangerere.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuwanusuru wananchi kutokana na madhara ya wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo yote yanayopakana na maeneo ya hifadhi. Utekelezaji wa mikakati hiyo unaendelea ambapo katika Wilaya ya Bunda yafuatayo yamefanyika:-
a) Umeanzishwa ushirikiano wa kudhibiti wanyamapori waharibifu kati ya watumishi kutoka Kikosi Dhidi ya Ujangili Bunda, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Pori la Akiba Ikorongo - Gurumeti, Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti na Mwekezaji Gurumeti Reserve;
b) Kutafuta vitendea kazi kwa ajili ya doria za wanyamapori waharibifu;
c) Vikundi 83 vimeanzishwa kwenye vijiji vinavyopakana na maeneo ya hifadhi kwa ajili ya kuchukua hatua za awali za kudhibiti wanyamapori hao pindi kunapokuwa na matukio ya wanyamapori waharibifu, wakati wakisubiri msaada wa Askari Wanyamapori;
d) Wizara imetoa tochi 100 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bunda. Mwanga mkali husaidia kufukuza tembo usiku kwa vijiji vinavyounda vikundi hivyo vya kufukuza wanyamapori;
e) Mafunzo kwa wananchi juu ya mbinu za kukabiliana na wanyamapori waharibifu yametolewa kwa vijiji, sambamba na kuwashauri kuepuka kulima kwenye shoroba za wanyamapori;
f) Kuweka madungu (minara) ambayo Askari Wanyamapori wanaitumia kufuatilia mwenendo wa tembo;
g) Kutumia teknolojia ya mizinga ya nyuki ambayo imewekwa pembezoni mwa mashamba; na
h) Mpango wa kutumia ndege zisizo na rubani kwa ajili ya kufukuza tembo unaendelea.
Mheshimiwa Spika, lengo la mikakati hii ni kuhakikisha kwamba, matukio ya uvamizi wa tembo yanashughulikiwa kwa haraka iwezekanavyo. Sambamba na mikakati hiyo Wizara imekuwa ikitoa fedha za kifuta jasho au kifuta machozi pale ambapo mazao yameharibiwa au wananchi wamejeruhiwa au kuuawa na wanyamapori wakali, akiwemo tembo.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwezi Machi hadi mwezi Oktoba, 2017, Wizara imelipa kifuta jasho na kifuta machozi cha jumla ya Sh.249,741,250 kwa wahanga 1,284 na vijiji 14 katika Wilaya ya Bunda.
Mheshimiwa Spika, sababu kubwa inayosababisha matukio ya wanyamapori wakali na waharibifu kuendelea kuwepo ni kuzibwa kwa shoroba na mapito ya wanyamapori. Kutokana na hali hiyo Serikali ina mpango wa kufufua shoroba za wanyamapori katika maeneo mbalimbali nchini kwa mujibu wa Kanuni za Shoroba, GN. 123 ya tarehe 16 Machi, 2018. (Makofi)