Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 42 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 358 2018-06-01

Name

Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Primary Question

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-
Wilaya ya Lushoto imezungukwa na misitu lakini misitu mingi imeungua kwa moto:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kurudisha uoto ule wa asili uliopotea kutokana na misitu kuungua?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shaabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, misitu iliyoungua moto katika kipindi cha kuanzia Agosti, 2016 hadi Februari, 2017 ni mitano ambayo ina jumla ya hekta 357.05 kati ya misitu 11 ambayo ina jumla ya hekta 22,855. Misitu hiyo ni Msitu wa Hifadhi Asilia Magamba wenye jumla ya hekta 9,381, zilizoungua ni hekta 338; Msitu wa Mkussu wenye hekta 3,674, zilizoungua ni hekta 3.8; Msitu wa Shagayu wenye hekta 7,830, zilizoungua ni hekta 2.75; Msitu wa Baga I wenye hekta 3,572, zilizoungua ni hekta 12; na Msitu wa Ndelemai wenye hekta 1,421, zilizoungua ni hekta 10.5.
Mheshimiwa Naibu Spika, misitu ya asili iliyoungua au kuharibiwa inaweza kurejeshwa kwa namna mbili. Mosi, kupanda miti maeneo yaliyoungua; na pili, kuliacha eneo liote miti lenyewe kwa kutofanya shughuli zozote za kibinadamu. Njia ya kwanza hutumika zaidi kwenye misitu ya kupandwa. Kutokana na asili ya eneo la Lushoto, njia nzuri zaidi ya kurudishia miti eneo lililoungua ni kuacha kufanya shughuli zozote za kibinadamu ili uoto wa asili urejee wenyewe. Aidha, kupanda miti isiyo ya asili ndani ya misitu ya hifadhi unaharibu uasilia wa msitu na huenda ukaleta matokeo hasi katika uoto wa asili uliopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia Wakala wa huduma za Misitu Tanzania unaendelea kutoa Elimu kwa jamii ili wananchi wanaoishi jirani na misitu ya hifadhi wawe makini wanapotumia moto wakati wa kusafisha mashamba yao, kwani chanzo kikuu cha moto wote uliounguza misitu katika kipindi hiki umetokana na wananchi kutayarisha mashamba yao bila kuchukua hatua za tahadhari.