Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 50 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 426 2018-06-13

Name

Athumani Almas Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Kaskazini

Primary Question

MHE. ALMAS A. MAIGE aliuliza:-
Zahanati ya Migungumalo, Kata ya Usagari Uyui ilijengwa kwa maandalizi ya kuwa Kituo cha Afya na kufunguliwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa tarehe 25/11/1997 na kuahidi kuwa zahanati hiyo itakuwa Kituo cha Afya cha Kanda ya Magharibi.
(a) Je, Serikali ina mipango gani ya kuikuza zahanati hiyo ili iwe Kituo cha Afya kutokana na mahitaji na huduma zinazotolewa kuwa juu ya uwezo wa zahanati?
(b) Kwa kuenzi kazi na juhudi za Rais Mstaafu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, kufika mpaka Usagari kufungua zahanati; je, Waziri yuko tayari kumwomba Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano kuja kuzindua Kituo cha Afya baada ya kuipandisha hadhi Zahanati hiyo ya Migungumano?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa Zahanati ya Migungumalo inahudumia wananchi na inatoa huduma za kiwango cha juu. Zahanati hii imeendelea kutengewa fedha kwa ajili ya kutoa huduma za afya kwa wananchi kupitia Mfuko wa Pamoja wa Afya, fedha za matumizi mengineyo, fedha za Benki ya Dunia (RBF), Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) na fedha za dawa kupitia Bohari ya Dawa (MSD). Lengo la Serikali ni kuendelea kuiwezesha zahanati hiyo iendelee kutoa huduma nzuri zaidi kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, miundombinu iliyopo kwa sasa katika Zahanati ya Migungumalo haikidhi vigezo vya kutoa huduma za afya kwa ngazi ya kituo cha afya. Kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kujenga vituo vipya na kuboresha vituo vya afya vilivyopo nchi nzima ili kuimarisha utoaji wa huduma kwa wagonjwa zikiwemo huduma za dharura na upasuaji.
Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali inaendelea na ujenzi wa vituo cha afya 210 kikiwemo Kituo cha Afya cha Upuge ambacho kimepokea shilingi milioni 500 ili kukiwezesha kutoa huduma za dharura na upasuaji. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ya Wilaya ya Tabora/Uyui imetengewa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambayo ikikamilika itahudumia wananchi wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge ashirikiane na Serikali ya Wilaya, Halmashauri na viongozi wa Kata ya Usagari ili waanze juhudi za kujenga Kituo cha Afya cha Kata ya Usagari na ikiwezekana waanze juhudi za kujenga zahanati katika kila kijiji kama sera ya afya inavyoelekeza. Serikali iko tayari kuunga mkono nguvu za wananchi katika kumalizia ujenzi huo utakaofanyika chini ya uratibu wa halmashauri, ofisi ya Mbunge na ofisi ya Mkuu wa Wilaya. Kuja kwa Mheshimiwa Rais au kiongozi mwingine wa kitaifa itategemea sana na aina ya miradi itakayokamilika. (Makofi)