Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 49 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 418 2018-06-12

Name

Hasna Sudi Katunda Mwilima

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kigoma Kusini

Primary Question

MHE. HASNA S. MWILIMA aliuliza:-
Wananchi wa Humule, Ubanda, Tandala na maeneo mengine ya Itebula wamekuwa wakisosa maeneo ya kulima kwa madai kuwa wanaingilia maeneo ya hifadhi:-
• Je, Serikali haioni sasa ni muhimu kusogeza mipaka kwa kushirikiana na TAMISEMI ili wananchi wapate maeneo ya kulima?
• Je, ni lini Serikali itamaliza usumbufu wanaoupata Wananchi wa Kijiji cha Kalilani kwa kudaiwa kuwa wamo ndani ya Hifadhi wakati Kijiji hiki kimesajiliwa kwa mujibu wa sheria?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hasna Sudi Katunda Mwilima, Mbunge wa Kigoma Kusini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
• Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya Humule, Ubande, Tandala na Itebula ni vitongoji ndani ya Kijiji kipya cha Lufubu kilichozaliwa ndani ya kijiji cha Kashagulu, Kata ya Kalya, Wilaya ya Uvinza ambacho kinatambulika kisheria. Eneo tajwa lilifanyiwa Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi mwaka 2006. Mchakato wa kuidhinisha mipaka ya ramani ya kijiji ulikamilika mwaka 2007 na ramani hiyo kusajiliwa kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji kama Kashagulu pia kilifanya mpango wa kurasimisha msitu wao wa kijiji wenye ukubwa wa hekta 38,313 kupitia mchakato shirikishi kama ilivyoelekezwa kwenye Sheria ya Misitu Na.14 ya 2002. Eneo hili ni vyanzo vya maji na linatambuliwa kama mapito ya wanyamapori yaani (Ushoroba) hususani tembo, nyati, sokwe na wengine wahamao kutoka Hifadhi ya Taifa Mahale kwenda Hifadhi ya Taifa Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuongeza maeneo ya kilimo lazima lifanyike kisheria kwa kuwa Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi uliidhinishwa na mkutano mkuu wakati huo. Mpango huo uliangalia matumizi ya wakati huo na ya baadaye kwa miaka 10 mpaka 15 ijayo.
• Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi ya Taifa ya Milima ya Mahale ilitangazwa rasmi katika GN Na. 262 ya tarehe 14 Juni, 1985. Maeneo ya Kalilani ni muhimu sana kwa uhifadhi wa sokwe, tembo, wanyama wengine pamoja na mazalia ya samaki. Aidha, wakati hifadhi hii inatangazwa, eneo hilo lilikuwa na wananchi jamii ya Watongwe waliopisha kutangazwa Hifadhi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Kalilani kilisajiliwa tarehe 5 Juni, 1995 ikiwa ni miaka takriban 10 baada ya Hifadhi ya Taifa kutangazwa. Wakati huo wavuvi wachache waliobakia eneo la Kaskazini Magharibi mwa hifadhi hii walianzisha kitongoji na baadaye kijiji kinachofahamika sasa kama Kalilani. Hii inadhihirisha kuwa eneo ambalo wanakijiji wanadai kuwa ni sehemu ya kijiji bado kisheria ni sehemu ya Hifadhi ya Mahale.