Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 48 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 405 2018-06-11

Name

Martha Jachi Umbulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-
Changamoto ya fedha za mikopo inayotolewa na Halmashauri za Wilaya kwa makundi ya wanawake na vijana nchini ni urejeshaji hafifu pamoja na kutorejeshwa kwa fedha hizo kabisa; kuna taasisi za fedha hapa nchini zinatoa mikopo kwa makundi tajwa hapo juu kwa ufanisi mkubwa na kwa uzoefu wa muda mrefu:-
Je, kwa nini Serikali isipitishe utoaji wa mikopo hiyo kwenye taasisi hizo zenye ufanisi wa muda mrefu na watalaam wa kutosha kama WEDAC ili kuepusha upotevu wa fedha za Serikali na mikopo kuwafikia walengwa?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali ilianzisha Mfuko wa Wanawake na Vijana baada ya kubaini kuwa wanawake na vijana wanashindwa kupata mikopo kutoka taasisi zingine za fedha ambazo zina masharti magumu. Lengo la kuanzishwa kwa mfuko huu ni kuondoa tatizo hilo ili kuwawezesha wanawake na vijana wengi kuendesha shughuli zao za kiuchumi ili kujikwamua na umaskini.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa taasisi zote za fedha hufanya biashara, unapoingia ubia na taasisi yoyote ya fedha lazima kuwepo na gharama za usimamizi wa mikopo hata kama masharti yatakuwa nafuu. Gharama hizo zinabebwa kwenye riba ukiacha masharti mengine kama dhamana na kadhalika. Kwa kuzingatia lengo la kuanzishwa kwa mfuko huo ambapo tunawalenga wananchi wa chini kabisa ambao hata uwezo wa kugharamia gharama za uendeshaji wa mifuko hiyo kwa wengine ni vigumu, ni vema mfumo wa uendeshaji uliopo na usimamizi chini ya Halmashauri ukaendelea kutumika.
Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge hili nawaelekeza Wakurungezi katika Halmashauri zote, kuhakikisha fedha zilizotengwa kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake na Vijana zinatolewa na kukopeshwa kwa vikundi hivyo kama ilivyoelekezwa katika mwongozo wa mipango na bajeti. Fedha hizo zitolewe kwa kadri mapato ya ndani yanavyokusanywa.