Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 47 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 399 2018-06-08

Name

Naghenjwa Livingstone Kaboyoka

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Kwa kuwa Ripoti za Ukaguzi za Ufanisi unaofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali zimeonesha kuna mapendekezo yanayotolewa baada ya ukaguzi mengi hayafanyiwi kazi na kwamba upungufu unaoibuliwa hujirudia mwaka hadi mwaka.
(a) Je, Serikali inakubaliana na pendekezo la kuanzisha kitengo maalum kitakachoratibu utekelezaji wa mapendekezo ya kaguzi za ufanisi?
(b) Je, Serikali inakubaliana na pendekezo kuwa baada ya Kamati ya PAC kujadili taarifa ya Ukaguzi wa Ufanisi ipeleke maoni yao kwa Kamati za Kisekta ili kutoa fursa kwa Kamati hizo kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mapendekezo ya CAG hasa katika maeneo ya kisera na kiutendaji kwa mujibu wa Kanuni za Bunge?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ukaguzi wa ufanisi wa miradi unaratibiwa na kufanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambaye hutoa mapendekezo yanayohitajika kutelekelezwa na wakaguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya taarifa ya kaguzi za ufanisi kukamilika, huwasilishwa Bungeni na Waziri mwenye dhamana na sekta husika, mfano Kilimo, Elimu, Maji na kadhalika, tofauti na ilivyo kwa taarifa za Ukaguzi wa Serikali Kuu na mashirika ya umma, ambapo taarifa zake huwasilishwa Bungeni na Waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha na taarifa ya kaguzi za Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwasilishwa Bungeni na Waziri mwenye dhamana na masuala ya Mamlaka za Serikali za Mitaa. Vilevile utekelezaji wa mapendekezo ya taarifa za ufanisi (performance audit) huratibiwa na Wizara husika. Wizara za kisekta ndizo ambazo hufuatilia na kuhakikisha kuwa mapendekezo ya CAG yanafanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na maelezo haya, haitakuwa vyema kuanzisha kitengo maalum cha kuratibu utekelezaji wa mapendekezo ya Taarifa ya Ukaguzi wa Ufanisi kwani kwa kufanya hivyo ni kuongeza gharama za uendeshaji wa Serikali. Hata hivyo Wizara, Idara au taasisi zinatakiwa kuwa na mpango kazi wa kuhakikisha kuwa mapendekezo yanayotolewa na CAG kupitia taarifa hizo, yanatekelezwa ipasavyo. Aidha, kupitia taarifa hizo za ufanisi, kunakuwa na masuala ambayo utekelezaji wake ni wa muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali siku zote ipo tayari na inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba, Sheria na Kanuni zilizowekwa zikiwemo Kanuni za Bunge. Hata hivyo, Serikali haina mamlaka ya kupanga au kuingilia majukumu yanayopaswa kutelekezwa na Kamati za Kudumu za Kisekta za Bunge. Hivyo basi, Bunge lako tukufu lina nafasi ya kuamua juu mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge.