Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 44 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 371 2018-06-05

Name

Ester Michael Mmasi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. ESTER M. MMASI) aliuliza:-
Kituo cha Afya Wilaya ya Siha kimeonekana kukidhi mahitaji yote muhimu tayari kwa usajili lakini hadi sasa kituo hicho hakijapata usajili wa Hospitali ya Wilaya.
Je, ni nini kauli ya Serikali katika kupandisha hadhi kituo hicho ili kupunguza kadhia ya upatikanaji wa huduma za kiafya kwa wananchi wa Wilaya ya Siha?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Michael Mmasi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuanzishwa Wilaya ya Siha haikuwa hospitali ya wilaya, hivyo Kituo cha Afya Siha ndicho kilichotumika kutoa huduma za matibabu kwa ngazi ya Hospitali ya Wilaya. Mwaka 2009/2010 Wilaya ya Siha ilipata eneo ambalo lilitolewa na vyama vya ushirika viwili ambavyo vilitoa jumla ya ekari 40 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, hii ilitokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Siha na hivyo kushindwa kumudu idadi ya wagonjwa na kupelekea uhitaji wa uanzishwaji wa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na wadau wengine wa maendeleo walisaidia uanzishwaji wa ujenzi wa Hospitali ya Wilayana kufikia kuanza kutoa huduma za afya. Hospitali inapokea wagonjwa wa rufaa kutoka katika vituo 20 vya kutolea huduma za afya vikiwemo vituo binafsi, vituo vya mashirika ya dini pamoja na vituo vya Serikali. Lengo la Serikali si kukipandisha hadhi Kituo cha Afya Siha kuwa Hospitali ya Wilaya, bali kuendelea kuboresha miundombinu inayoendelea kujengwa katika Hospitali ya Wilaya ili kuwa na hadhi kamili ya kupata usajili kama Hospitali ya Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendelea kuboresha huduma Serikali katika mwaka wa fedha 2016/2017 ilitoa shilingi milioni 250 ambazo zimetumika kumaliza jengo la wagonjwa wa nje ambalo ukamilishaji wake uko hatua za mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuendelea kuboresha miundombinu ya hospitali hiyo ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi. Aidha, Halmashauri kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Siha imeomba wadau mbalimbali ambao wameweza kuchangia jumla ya shilingi milioni 129.38 kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya akina mama ambayo iko katika hatua za umaliziaji.