Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2000-2005 Session 12 Sitting 8 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 101 2018-09-13

Name

Silafu Jumbe Maufi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SILAFU J. MAUFI aliuliza:-
Serikali inafahamu kuwa michezo ni afya na ni ajira pia, lakini mikoa kadhaa hapa nchini ina viwanja visivyokidhi hadhi ya kitaifa na kimataifa na hata kasi ya kuibua vipaji vipya imedorora katika Mikoa ya Rukwa, Tabora, Iringa, Kigoma na kadhalika.
Je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kushirikiana na wamiliki wa viwanja hivyo kuvikarabati na kuviboresha kufikia hadhi stahiki?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. ANTHONY P. MAVUNDE K.n.y. WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silafu Jumbe Maufi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kwamba ujenzi wa miundombinu ya michezo ni jambo muhimu sana katika kuendeleza vipaji vya wanamichezo na ndiyo sababu ya Serikali kujenga viwanja changamani vikubwa viwili nchini ambavyo ni Kiwanja cha Uhuru na Kiwanja cha Taifa, Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, maandalizi ya kazi ya ujenzi wa kiwanja kikubwa cha Ngamani cha tatu Jijini Dodoma yanaendelea. Hata hivyo Serikali haiwezi peke yake kujenga miundombinu ya kisasa kwa michezo yote bila mchango wa Halmashauri zetu, taasisi za umma, asasi na kampuni binafsi na vilevile mashirikisho na vyama husika vya michezo mbalimbali hapa nchini.
Mheshimiwa Spika, pale penye jitihada bayana za kujenga miundombinu ya michezo, Serikali daima imekuwa mstari wa mbele kusaidia juhudi hizo. Utaratibu mkubwa wa viwanja vya Kaitaba - Kagera na Nyamagana - Mwanza, ni matokeo ya mazingira mazuri ya ushirikishaji yaliyowekwa na Serikali kati ya wadau soka, Shirikisho la Soka nchini na Shirikisho la Soka la Dunia.
Aidha, ukarabati mkubwa wa viwanja vya Namfua - Singida; Samora Machel - Iringa na Majaliwa Stadium - Ruangwa ni matokeo ya mazingira mazuri ya ushirikiano yaliyowekwa na Serikali kati ya wadau, TFF na Wizara yenye dhamana ya michezo. Naomba nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mbunge) kwa kuonesha mfano wa kuhamasisha Halmashauri yake na wananchi wa Ruangwa kuunganisha nguvu na kujenga uwanja wa Majaliwa Stadium. (Makofi)